Nyani na Mamba walikuwa marafiki wa dhati.
Walicheza pamoja. Walikula pamoja. Walifanya kila kitu pamoja.
Siku moja, Mamba alikuwa mgonjwa mahututi. Alikuwa karibu kufa.
Mamba alienda kwa mkanga. "Kama unataka kupata nafuu, itakubidi ule nyama ya Nyani," mkanga akamwambia.
Aliposikia haya, Mamba alilia.
Kama angetaka kupata nafuu, hakuwa na jingine ila kumla rafikiye, Nyani.
Nyani alipoenda kumwona rafiki yake Mamba, aliupanda mgongo wake.
Mamba alimpeleka Nyani mtoni kwenye maji mengi.
"Ni nini kinachokutatiza, rafiki yangu?" Nyani aliuliza.
Mamba alisema, ''Mkanga aliniambia kuwa kama ninataka kupata nafuu lazima nikule wewe, rafiki yangu."
Nyani akajibu, "La hasha! Huwezi kunila. Mimi ni mdogo mno!
Subiri nimwite babu yangu. Ni mkubwa kuniliko mimi. Ukimla yeye utashiba."
Mamba akauliza, "Yu wapi huyu babu yako?"
Nyani akajibu, "Yuko mtini kule kisiwani."
Mamba akasema, "Nenda ukamlete ili nimle."
Nyani aliruka na kukimbia moja kwa moja hadi mtini.
Mamba akangoja na kungoja lakini Nyani hakurudi.
Na huo ndio ukawa mwisho wa urafiki wao.