Mto wa Upinde wenye miujiza
Mimi Werna
Edwin Irabor

Watoto watatu, Ado, Aggie, na Eddy waliisikiliza mvua ikinyesha. Walitaka sana kuchezea kwenye mvua hiyo. Walitaka kuugusa upinde ulioonekana angani. Lakini mama alisema, "La!"

Walilia wakitumaini kwamba mama atabadili nia yake. Lakini, hilo halikufanyika. Eddy hata alijaribu kunyatia na kutoka nje ya nyumba ili autembelee upinde ule.

1

Mama alimpata kabla hajaenda mbali. Aliipaza sauti yake ili Eddy na dada zake pia waweze kusikia.

"Utapata mafua," mama alisema. "Hampendi kunywa supu iliyo na pilipili lakini mkipata mafua, lazima mtainywa," aliongezea kwa tabasamu.

2

Akiwa na matumaini kwamba watamwuliza awasimulie hadithi, mama alisema, "Upinde ni mto wa miujiza ulio na nguvu za kuponya. Lakini upo mbali angani msikoweza kuufikia. Kwa hivyo mkipata mafua, upinde hautawasaidia."

3

"Tafadhali, mama, tusimulie ile hadithi inayohusu upinde," Aggie alisema. "Ndiyo, tafadhali, mama, ningependa kuisikia pia," Ado aliongeza. "Mimi pia," Eddy alimsihi mama huku akimvuta mkono.

"Hebu tuone, mmmm," mama alisema kwa utani. "Sawa wapendwa, karibieni. Mama yenu msimulizi ndiye huyu hapa kuwasimulia!"

4

Aggie aliileta fimbo iliyotumiwa na wasimulizi. Alimpatia mama. Eddy alikileta kitambaa alichozoea kuvaa aliposimulia. Alipoishika ile fimbo na kukivaa kile kitambaa, mama alikuwa tayari kuwasimulia wanawe hadithi.

Waliketi kimya kuisikiliza ile hadithi waliyoisikia mara nyingi. Ado aliipuliza firimbi kuashiria kuanza. Kisha masimulizi yalianza.

5

"Hapo zamani, upinde ulikuwa mto wa miujiza. Ulikuwa umejificha katika vichaka vilivyokuwa kijijini Bombo. Kwa sababu ulikuwa na nguvu za kuponya, ulipewa ulinzi mkali. Yeyote aliyekuwa mgonjwa, aliyanywa maji yake.

Upinde huo ulifurahi ulipogawanya nguvu zake. Lakini haukupenda watu wasiokuwa na nidhamu."

6

"Kwa sababu ya nguvu zake za miujiza, kulikuwa na aiskrimu kwenye ukingo wa mto huo! Waliokuja kuyanywa maji, hasa watoto, vilevile walifurahi kuila aiskrimu.

Aiskrimu hiyo ilikuwa ya rangi nyekundu, rangi ya machungwa, manjano, kijani kibichi, bluu, zambarau na nili."

7

"Siku moja, Bomu, Bi kizee mmoja mtukutu, alikuja kutoka nchi ya mbali. Alipowasili, alikutana na mlinzi. Mlinzi hakumtambua kwa hivyo alikuwa na hisia asizowahi kuwa nazo. Hata hivyo, alizipuuza hisia zake.

Alimwelekeza Bi kizee huyo kwenda mtoni huku akimkumbusha kuuheshimu ule mto. Bomu alikubali kisha akaenda majini."

8

"Bomu aliyanywa maji na akapona. Halafu akatazama kuhakikisha kwamba hakuna aliyemwona. Alilichukua jiwe akalitumbukiza majini.

Alilitazama likiinuka na kusambaza viwimbi vyake. Alifurahi sana hata akakichukua kijiti na kurudia kitendo hicho. Vilevile, kijiti kilisambaza viwimbi vyake."

9

"Bomu aliruka majini! Alikuwa na matumaini ya kuupata uzima wa milele. Mara tu aliporuka, mto uliinuka juu. Uliruka juu angani, usiwahi kurudi tena kijijini Bombo.

Wakati mwingine, upinde hutokezea baada ya mvua na kuonekana kama mto tena. Na huo ndio mwisho wa hadithi yangu," mama alisema.

10

"Kwa hivyo, wapenzi wangu, niambieni, kwa nini mnaipenda sana hadithi hii?" mama aliuliza. "Kila mara mnaniuliza niwasimulie."

Ado alitabasamu kisha akajibu, "Ninaipenda kwa sababu inanikumbusha kuzisikiza hisia zangu."

Naye Aggie akasema, "Inanikumbusha rangi za upinde."

11

Eddy alijaribu bahati yake, "Ninaipenda kwa sababu inanikumbusha aiskrimu! Tafadhali, ninaweza kupata aiskrimu kidogo sasa?"

"Mmmm. Sasa kuna baridi sana. Heri tuile aiskrimu kesho," mama alisema. Kisha akaongeza, "Wakati ujao, nitawaeleza hadithi kuhusu hatima ya upinde."

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mto wa Upinde wenye miujiza
Author - Mimi Werna
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Edwin Irabor
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs