Katika kijiji kimoja, watu walitofautiana kuhusu kazi gani iliyo muhimu.
Kila mmoja aliamini kuwa kazi yake ndiyo iliyokuwa muhimu zaidi!
Mwalimu alisema kazi yake ndiyo iliyokuwa muhimu zaidi.
"Bila walimu, hakuna yeyote atakayeweza kwenda shule kujifunza."
Mjenzi akasema kwamba kazi yake ndiyo iliyokuwa muhimu zaidi.
"Bila wajenzi, hakungekuwa na shule za kusomea wala nyumba za kulala."
Seremala naye akasema kwamba yeye ndiye aliyekuwa na kazi muhimu zaidi.
"Bila maseremala, hakungekuwa na samani
za kutumia nyumbani na shuleni."
Daktari naye alidai kuwa alikuwa na kazi iliyo muhimu kuliko zote.
"Bila madaktari na wauguzi, watu wangeugua na kufa."
Mkulima akasema kwamba kazi yake ni muhimu zaidi.
"Bila wakulima, hakungekuwa na chakula."
Mwanafunzi naye alisema kuwa wanafunzi ndio walio na kazi muhimu kwa zote.
"Bila wanafunzi, hakungekuwa na walimu, wajenzi, madaktari, wakulima, wala maseremala."
Hatimaye, kila mmoja alikubali kwamba
kazi zote ni muhimu. Tunahitaji walimu, wajenzi, madaktari, wakulima, na maseremala.
Lakini, lazima kila mmoja awe mwanafunzi kwanza!