Kuhesabu Kabichi
Penelope Smith
Magriet Brink

Mama Koki amekuwa akichuma kabichi wiki nzima. Dona, Maya na Duki humsaidia Mama Koki katika bustani yake kila Jumamosi asubuhi.

Leo watoto hawa watahesabu na kupakia kabichi. Baba Koki atayapeleka masanduku yaliyojaa kabichi sokoni kuuza.

1

Teksi iliwafikisha watoto kwenye lango la bustani. Waliliona rundo kubwa la kabichi karibu na gari la Baba Koki.

"Salala! Kabichi nyingi kweli!" Maya alishangaa. "Bila shaka kuna kabichi elfu moja hapo!" Duki alicheka.

"La! Hasha! Pengine ni mia mbili tu!" Dona alipinga.

2

Mama Koki alikuwa amewasubiri langoni. "Hamjambo, nimefurahi kuwaona!" Aliwasalimu watoto.

"Hebu tuanze kazi. Mtahesabu na kuweka kabichi kumi na mbili katika kila sanduku. Nina masanduku 20. Wawili kati yenu watapakia kwenye masanduku 7 kila mmoja. Aliyebaki, atapakia kwenye masanduku 6."

3

Watoto walilitazama lile rundo la kabichi. Wakajadili njia tofauti za kuzihesabu kabichi hizo.

"Mimi nitahesabu zangu mbili mbili," Maya akasema.

"Ninapenda kuhesabu nne nne. Ni haraka," Duki akajibu.

"Mimi nitazihesabu tatu tatu ili niwe tofauti nanyi!" Dona akawajibu.

4

Watoto walijaza masanduku yote 20. "Kazi nzuri!" Mama Koki aliwapongeza. "Tazama, kabichi zimezalia. Nguruwe wangu wanazipenda. Hebu tuwagawie," Mama Koki aliamua.

"Mlipakia jumla ya kabichi ngapi katika masanduku yote? Ni kabichi ngapi zilizalia?" aliwauliza watoto.

5

Waliandika bei kwenye kila sanduku. Halafu, wakamsaidia Baba Koki kuyapakia kwenye gari.

Waliweka nusu ya masanduku upande mmoja. Na nusu nyingine upande wa pili ili uzito ulingane.

6

"Karibu tukamilishe kazi!" Baba Koki alisema. "Hebu tuone ni masanduku mangapi tunahitaji kuweka kila upande."

7

Muda mfupi baadaye, masanduku yote 20 yalikuwa yamepakiwa kwenye gari. Baba Koki aliondoka kwenda sokoni.

Aliwaza, "Nikifaulu kuuza masanduku yote, nitapata pesa za kutosha. Nitaweza kuwashangaza watoto kwa kurekebisha zizi la nguruwe!"

8

Nyumbani, Mama Koki na watoto walinyunyizia mimea maji na kukusanya majani. Kufikia saa sita, wote walikuwa wamechoka.

Mama Koki aliwaambia, "Ni wakati wa karamu yenu. Je, mnajua nilichowaandalia leo?"

9

Aliingia ndani kuwaletea alichokuwa amewaandalia. Watoto walisubiri kwa uvumilivu huku wakikisia atakacholeta.

Aliporejea, waliona mifuko ya aproni yake ikiwa imejaa!

10

"Hebu tuone ikiwa mlikisia sawa! Nimewatayarishia nini leo?" Mama Koki aliyaweka matofaa mezani. "Nilikisia sawa!" Duki alisema kwa furaha.

Mama Koki aliwaambia watoto, "Kumbukeni sharti! Gawanya sawa ili kila mmoja apate haki yake. Hakuna anayepata zaidi wala kidogo kuliko mwingine!"

11

Kwanza, watoto walihesabu matofaa mawili mawili. Walihesabu: 2, 4, 6, 8, 10, 12, 14, 16, na tofaa moja likabaki. Yote pamoja, yalikuwa matofaa 17.

12

Waligawana matofaa sawasawa yakabaki matofaa mawili.

Watoto waliyaweka matofaa yao mikobani ili waende nayo nyumbani kwao.

13

"Hebu tuyakate matofaa mawili yaliyobaki ili tugawane kati yetu," Duki aliwaambia.

"Kila mmoja wetu atapata vipande vingapi vya tofaa?" Maya aliuliza.

"Ninajua jibu!" Dona alitabasamu.

14

Wakati huo, Baba Koki alirejea nyumbani kutoka sokoni. Gari lilikuwa tupu naye alikuwa akitabasamu.

"Niliuza kabichi zote. Sasa ninaweza kurekebisha zizi la nguruwe. Nitaweza pia kuwanunulia ule mpira wa miguu mliotaka."

Watoto walishangilia, "Yee!"

15

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Kuhesabu Kabichi
Author - Penelope Smith
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Magriet Brink
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs