Mbio kuhimiza umoja wa Afrika
Ursula Nafula
Brian Wambi

Kadogo na Juma ni marafiki.

Wanapenda kukimbia pamoja kila siku.

1

Siku moja, Juma alisema, "Tukimbie kwa ajili ya bara letu, tuhimize umoja wa Afrika!"

"Sawa, twende!" Kadogo alikubaliana naye.

2

Waliamua kuibeba kurunzi ya umoja kwenye safari yao.

Walianzia mbio hizo katika upande wa kusini jijini Cape Town.

3

Kutoka Afrika Kusini, walielekea kaskazini kupitia magharibi mwa bara. Walipitia Namibia, Angola, Kongo na Cameroon.

Waliamua kupumzika jijini Abuja.

4

Wakimbiaji kutoka Afrika Magharibi walijiunga nao nchini Nigeria.

Waliendelea pamoja wakiufuata Mto Niger.

5

Walipofika Mali, walikumbwa na upepo mkali. Juma aliwashinda wote kwa nguvu.

Alijitwika jukumu na kuwaongoza salama.

6

Walipofika pwani ya Guinea, jijini Conakry, walikuwa wamejaa vumbi. Walienda kuogelea baharini.

Baadaye waliamua kuendelea na mbio zao kwenda Morocco kupitia Senegal na Mauritania.

7

Jijini Casablanca, wakimbiaji waliungana na vijana wenzao wakacheza ufukoni.

Halafu, wakaelekea Afrika Kaskazini.

8

Walikimbia kupitia Algeria na Libya wakapumzika Misiri ili wazitembelee piramidi.

Baadaye, waligeuka kusini wakaufuata Mto Nile kuelekea Uganda.

9

Walipita kwenye jangwa na mbuga za kitaifa. Vijana zaidi walijiunga nao jijini Kampala.

Kutoka Kampala, kikundi hicho kilielekea pwani ya Kenya.

10

Walipofika jijini Mombasa, waliketi ufukoni wakala wali wa nazi kwa samaki.

Juma alisema, "Hebu tuipeleke kurunzi ya umoja Mlimani Kilimanjaro."

11

Hata hivyo, Juma alikuwa amechoka. Walipokuwa njiani wakielekea Tanzania, alianguka chini.

Wakimbiaji wenzake walizikatiza mbio zao wakarudi nyuma kumsaidia Juma.

12

Juma alimpokeza Kadogo kurunzi akisema, "Ibebe kurunzi hii hadi Mlimani Kilimanjaro. Hakikisha umewasha mwale wa umoja wa Afrika."

13

Watu waliwashangilia wakimbiaji wakisema, "Ninyi ni mashujaa wetu."

Baada ya kuwasha mwale wa umoja Mlimani Kilimanjaro, walirejelea mbio kuelekea kusini mwa Afrika.

14

Walipofika Malawi, walikatiza mbio zao. Wakaenda kuogelea katika Ziwa Malawi.

Kadogo alimwambia Juma, "Tumekimbia kutoka kusini hadi kaskazini, mashariki hadi magharibi. Safari yetu inakaribia kukamilika."

15

Hatimaye, wakimbiaji wa umoja waliibeba kurunzi yao hadi nchini Zimbabwe. Umati wa watu ulikusanyika pale kushuhudia jambo hilo.

"Mbio zimefana kweli!" Alisema Juma huku akitabasamu.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mbio kuhimiza umoja wa Afrika
Author - Ursula Nafula
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Brian Wambi
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs