Mbweha na Sungura
Mohammed Kuyu
Jacob Kono

Hapo zamani za kale, kulikuwa na Mbweha aliyekuwa na njaa.

Alijaribu kumshika panya, lakini panya alitoroka.

1

Alijaribu kumfukuza kichakuro, lakini kichakuro pia alikimbia na kupanda juu ya mti.

Kisha Mbweha akamwona panya mdogo aliyenona. Akawaza, "Huyu anafaa kuliwa." Panya alipomwona Mbweha, alikimbilia chini ya jiwe, akaruka shimoni mwake.

Mbweha akawaza, "Ni lazima nichimbe nikamtoe panya huyu shimoni."

2

Mbweha alikimbilia chini ya jiwe hilo kubwa akaanza kuchimba. Alichimba ndani zaidi hata jiwe likamwangukia mguuni.

Alishindwa kuutoa mguu wake chini ya jiwe. Akapiga mayowe, "Nimenaswa! Nisaidie! Nisaidie!"

3

Sungura alipomsikia Mbweha akilia, alikimbia na kumwuliza, "Una nini?"

Mbweha akamjibu, "Nilikuwa nikiwinda panya kisha jiwe likaniangukia mguuni. Tafadhali mpendwa Sungura, nisaidie!"

4

Sungura alimjibu, "Mmmh! Ningependa sana kukusaidia lakini, mimi ni mdogo na hafifu na jiwe hili ni kubwa. Itakuwa vigumu kwangu. Je, utanipa nini nikikusaidia?"

Mbweha alilia aksema, "Jioni nitakupikia mlo uupendao. Utakula chakula kitamu kuliko vyote duniani."

Sungura alimjibu, "Sawa, nitajaribu kukusaidia."

5

Sungura alilisukuma jiwe, lakini, halikusonga hata kidogo.

Akalisukuma tena na tena hadi likauondokea mguu wa Mbweha. Sungura akafurahi.

6

Sungura akasema, "Nipe zawadi yangu."

Mbweha akamwuliza, "Zawadi gani? Umenona na unatamanika."

Sungura akamwuliza, "Si nimekusaidia? Wawezaje kutaka kunila?"

Mbweha akajibu, "Mbweha hula sungura. Usibishane nami."

Sungura akasema, "Hiyo si haki. Tuwatafute wazee watupe mawaidha yao."

7

Sungura na Mbweha walimpata mzee mmoja.

Sungura akasema, "Tafadhali tusaidie. Mbweha anataka kunila ilhali niliyaokoa maisha yake. Jiwe lilikuwa limemwangukia mguuni na hangeweza kujitoa. Aliniahidi chakula kitamu cha jioni. Nami nikalisukuma jiwe na kuliondoa mguuni pake. Sasa ameisahau ahadi yake."

8

"Si sawa. Mbweha, kwani huna shukurani? Mwache Sungura aende zake," Mzee alinena.

Mbweha alikifungua kinywa chake akamwonyesha Mzee meno yake marefu na makali. Kisha akasema, "Hapana! Sitamwachilia aende. Na usijaribu kunizuia au nitakukula wewe pia."

9

Mzee aliogopa sana akasema, "Tafadhali usinile. Labda, nimefanya uamuzi usio sawa. Unayoyasema ni kweli. Siwezi kuamua ilhali sikuliona jiwe. Je, ni nini hasa kilichofanyika?"

10

"Hilo ni jambo rahisi. Twende nikuonyeshe," Mbweha akasema.

Mzee alikwenda pamoja na Mbweha na Sungura kuliona jiwe. Kisha akamwuliza Mbweha, "Kwani ulikuwa unafanya nini?"

11

Mbweha akaeleza, "Panya niliyekuwa nikimwinda alitorokea shimoni. Nilipokuwa nikilichimba shimo hilo, jiwe liliniangukia mguuni."

"Jiwe gani?" Mzee akauliza. "Jiwe hili," Mbweha akajibu.

"Wewe ulikuwa wapi?" Mzee akauliza. "Nilikuwa hapa," Mbweha akasema huku akijilaza chini.

12

Mzee alimtazama Sungura kisha akasema, "Wewe ni Sungura mdogo tu na hafifu. Siamini kuwa uliweza kulisongeza jiwe kubwa kama hili."

"Lakini nililisongeza!" Sungura alilia.

"Hebu nionyeshe," Mzee akasema.

13

Sungura alisukuma akasukuma. Jiwe likaungukia mguu wa Mbweha tena.

Mzee akauliza, "Hivi ndivyo ulivyompata Mbweha?"

Sungura akaitikia kwa kichwa.

14

Mzee akamwuliza Mbweha, "Je, Sungura alikupata katika hali hii?"

Mbweha aliitikia kwa kichwa.

Mzee akasema, "Vizuri. Hii ndiyo haki. Sungura, kimbia nenda zako nyumbani. Nami pia ninakwenda nyumbani."

15

Basi, Mzee na Sungura wakaondoka.

Wakamwacha Mbweha asiye na shukrani peke yake.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mbweha na Sungura
Author - Mohammed Kuyu, Elizabeth Laird
Translation - Susan Kavaya
Illustration - Jacob Kono
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs