Hapo zamani, Ngurumo na Radi waliishi duniani miongoni mwa watu.
Ngurumo alikuwa mamake Radi.
Radi alikuwa mwenye hasira kali.
Mara nyingi alibishana na mamake.
Radi alipokasirika, aliteketeza nyumba na kung'oa miti.
Alitoa sauti ya kutisha, "Pia-la-la-la, pia-la-la-la!"
Aliyaharibu mashamba na hata kuwaua watu.
Radi alipofanya vitendo hivi, mamake alimwita kwa sauti ya juu, "Bum-rambo-la-la-la, la-bum!"
Alijaribu kumzuia asisababishe uharibifu.
Radi hakutia maanani aliyosema mamake.
Badala yake angesababishia kila mmoja fujo alipokuwa na hasira.
Hatimaye, watu walipeleka malalamishi yao kwa mfalme.
Mfalme aliamrisha Ngurumo na mwanawe wahame kutoka kijijini.
Aliwafukuza waende kuishi mbali na makao ya watu.
Hili halikusaidia sana. Radi alizidi kuteketeza misitu alipokasirika, "Pia-la-la-la, pia-la-la-la!"
Wakati mwingine, ndimi za moto zilisambaa na kuunguza mashamba.
Kwa mara nyingine, watu Walienda kwa mfalme kumlalamikia.
Mara hii, mfalme aliwaambia Radi na Ngurumo kwamba hawangeendelea kuishi duniani.
Aliwafukuza waende kuishi angani wasikoweza kusababisha uharibifu mwingi.
Tangu wakati huo, Radi anapokasirika, huweza kuteketeza na kuharibu, "Pia-la-la-la, pia-la-la-la!"
Nasi bado tunamsikia Ngurumo, mamake Radi, akimkemea, "Bum-rambo-la-la-la, la-bum!"