Sungura na Fisi
Mutugi Kamundi
Rob Owen

Hapo zamani Sungura na Fisi walikuwa marafiki wa chanda na pete.

Walifanya kazi na kucheza pamoja.

1

Siku moja, Sungura alisema, "Rafiki, tuanze kulima pamoja ili tuwe tajiri."

"Ah, kweli, tunaweza kupanda vyakula vingi na kuviuza," Fisi alimjibu.

"Lakini, tutapanda nini?" Sungura aliuliza.

2

Fisi alipendekeza wapande mahindi. Sungura alikubali kisha akamwambia Fisi kuwa wagawane majukumu.

Sungura akasema, "Kazi yangu itakuwa kuwachunga ndege wasile mahindi."

Fisi naye akasema kuwa kazi yake itakuwa kulima shamba, kupanda na kupalilia.

3

Fisi alinung'unika kwamba alikuwa amepewa kazi nyingi. Sungura alisema kuwa kazi ya kuwafukuza ndege ndiyo ngumu zaidi na ya muhimu.

Alisema, "Kazi yangu si rahisi. Nitakwea miti na kuwafukuza ndege mchana na usiku. Wewe huwezi kufanya hivyo."

4

Fisi alikubaliana na Sungura. Alilima shamba peke yake. Baada ya kulima shamba lote, Fisi alipanda mahindi.

Ilikuwa kazi nyingi kweli!

5

Fisi alipokuwa akifanya kazi, Sungura aliketi na kuimba:

Rafiki yangu ni mfanya kazi, mimi ni mwelekezi. Anafanya kazi kama trekta, mimi ni meneja.
Udongo anaolima, milima anayolima, mbegu anazopanda, magugu anayokata, mahindi tunayovuna.

6

Mahindi yalistawi. Sungura aliimba kwa furaha huku akiwafukuza ndege.

Kazi yake ilikuwa rahisi. Hakutoa jasho hata kidogo.

7

Walipokuwa tayari kuvuna, Sungura alimwambia Fisi, "Nitavuna kila kitu kinachomea juu ya udongo nawe utavuna kila kinachomea chini ya udongo."

Fisi alidhani hilo lilikuwa wazo nzuri.

8

Sungura alimwambia Fisi, "Nitavuna yangu kwanza kisha wewe uvune yako."

Sungura alivuna mahindi yote na kuyahifadhi kwake.

9

Fisi alienda kuvuna vitu vyote vilivyokuwa chini ya udongo.

Hakupata mazao yoyote ila mizizi pekee.

10

Fisi aligundua kwamba alikuwa amedanganywa. Alirejea nyumbani kwa hasira na vikapu tupu.

Alimwambia Sungura, "Hebu rafiki yangu tulime pamoja mara nyingine."

11

Fisi aliongeza kusema, "Mara hii nitavuna kila kinachomea juu ya ardhi nawe utavuna kila kinachomea chini ya ardhi."

Sungura alikubali. Alisema kuwa badala ya kupanda mahindi ingekuwa heri kubadili na kupanda viazi.

12

Fisi pia alisizitiza kwamba mara hiyo wote watalima, wapande na wavune pamoja.

Sungura alikubali. Walifanya kazi shambani pamoja.

13

Viazi vilipokuwa tayari, Sungura alimwambia Fisi kuvuna vyote vilivyomea juu ya udongo.

Fisi alipata majani ya viazi pekee. Alirudi nyumbani na vikapu tupu.

14

Sungura alivuna viazi vingi. Fisi alipoona mavuno ya Sungura, alimwuliza kwa hasira, "Mbona ulinidanganya?"

Sungura alisema kuwa Fisi mwenyewe alichagua kuvuna vitu vilivyomea juu ya udongo.

15

Fisi alikasirika mno. Alimfukuza Sungura kutaka kulipiza kisasi.

Sungura alikimbia kwa kasi na kwenda zake. Tangu siku hiyo, Sungura na Fisi ni maadui.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Sungura na Fisi
Author - Mutugi Kamundi
Adaptation - Ursula Nafula
Illustration - Rob Owen
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs