Hakimu asiyekuwa na busara
Magabi Eynew Gessesse
Brian Wambi

Hapo zamani, waliishi majirani wawili marafiki, Meseret na Demeke. Walikuwa maskini sana.

Siku moja, Meseret alimwambia Demeke, "Lazima leo niipeleke ngano yangu sokoni. Gunia ni nzito na soko iko mbali. Ningekuwa na pesa za kutosha, ningemnunua punda."

1

Demeke alijibu, "Nami lazima nikavinunue vyungu vipya leo sokoni. Vitakuwa vizito mno. Heri ningekuwa na punda vilevile. Kwa sasa, ninazo tu nusu ya pesa."

2

Meseret alikuwa na wazo. Alisema, "Hebu tumnunue punda pamoja. Wewe utalipa nusu nami nilipe nusu. Nitamtumia kwenda sokoni kwa juma moja nawe umtumie kwa juma lingine."

Meseret na Demeke walimnunua punda. Kwa muda mrefu waliishi kwa furaha.

3

Siku moja, babake Meseret alifariki. Meseret alirithi mashamba, miti, ng'ombe na kondoo.

Alikuwa tajiri na hakutaka kufanya kazi na Demeke tena. Vilevile, alitaka nusu yake ya punda.

4

Meseret alimwambia Demeke, "Mbwa wangu wanahitaji nyama. Ninataka kumchinja punda wetu wewe uchukuwe nusu yake nami nichukuwe nusu itakayobaki."

Demeke alilia, "Sihitaji nyama yoyote ila punda. Ikiwa unataka kumchinja, nipe pesa za nusu yangu." Meseret alifoka, "Sitakupatia pesa zozote. Nusu ya punda ni yangu na ninaitaka sasa." Demeke alisema, "Hebu twende kwa hakimu atuamulie."

5

Meseret na Demeke walienda kumwona hakimu alisiyekuwa na busara. Hakuwasikiliza kwa makini. 

Hakimu aliwauliza, "Mnammiliki punda pamoja?" "Ndiyo," Meseret na Demeke waliitikia. Hakimu akasema, "Basi, kila mmoja atapata nusu. Iwapo Meseret anataka nusu yake, ana haki ya kuichukuwa. Mchinjeni punda kisha mmgawe nusu mbili."

6

Meseret alifurahi. Alimchinja punda na kuchukua nusu ya nyama kuwapelekea mbwa wake.

Demeke alihuzunika akawaza, "Maskini punda wangu hayupo tena, na sasa lazima nibebe kila
kitu mwenyewe."

7

Baadaye, Meseret alitaka kujijengea nyumba mpya. Alifikiri, "Nitakiteketeza chumba changu kizee kisha niijenge nyumba mpya nzuri na kubwa." Meseret alivihamisha vitu kutoka chumbani.

Demeke alimwuliza, "Unafanya nini?" Meseret alimjibu, "Ninataka kukiteketeza chumba changu ili niijenge nyumba mpya."

Demeke alikuwa na wasiwasi, "Lakini, chumba chako ki karibu na changu. Ukikiteketeza, changu pia kitateketea."

8

Kwa hasira, Meseret alisema, "Usijaribu kunizuia! Hiki ni chumba changu na nikitaka nitakiteketeza." Demeke alilia, "Wacha! Hebu twende tumwulize hakimu."

Kwa sababu hakimu hakuwa mwenye busara, hakusikiliza kwa makini wala hakuelewa. Hatimaye alisema, "Meseret ana haki ya kukiteketeze chumba chake na hakuna anayeweza kumzuia."

9

Meseret alipokiteketeza chumba chake, upepo uliupeperusha moto hadi kwenye paa la chumba cha Demeke. Punde, chumba chake pia kilianza kuteketea.

Demeke alimlilia hakimu, "Tazama! Meseret amekiteketeza chumba changu! Lazima anilipe." Hakimu aliamua, "La! Meseret alikiteketeza chumba chake. Moto ndio uliokiunguza chumba chako. Meseret hastahili kukulipa."

10

Maskini Demeke alihuzunika sana. Hakuwa na punda wala chumba. Alibaki na shamba peke yake.

Kila siku alifanya kazi shambani mwake na usiku kulala chini ya mti.

11

Demeke alifanya kazi kwa bidii shambani mwake. Aliyang'oa magugu na kuwafukuza ndege.

Wakati wa kuvuna ulipofika, kulikuwa na mazao mazuri ya mbaazi.

12

Siku moja, wanawe Meseret walipitia katika shamba la Demeke.

Waliona mbaazi wakasema, "Mbaazi ni tamu sana!" Walizivamia wakazitoa zote.

13

Demeke alipowaona wanawe Meseret, aliwaambia, "Nirudishieni mbaazi zangu."

Walimjibu kwa dharau, "Hatuwezi kukurudishia kwa kuwa tumezila. Mwulize baba akulipe."

14

Demeke alimwambia Meseret, "Wanao wamezila mbaazi zangu." Meseret alimjibu, "Nitakupa pesa."

"Sitaki pesa zako. Ninataka mbaazi zangu." Demeke alitishia. 

"Subiri! Hebu twende tumuulize hakimu," Meseret alilia.

15

Meseret na Demeke walimwona hakimu yule yule. Kama kawaida, hakuwasikiliza kwa makini wala hakufikiria juu ya tukio hilo. "Wanawe Meseret walikula mbaazi zako na ni lazima zirudishwe. Pasua tumbo zao uchukuwe mbaazi zako." Hakimu aliamua. 

Meseret alisononeka sana akasema, "Wanangu watafariki! Tafadhali, Demeke, nitakupatia pesa." "Nilitaka pesa ulipomchinja punda wetu. Ninataka mbaazi zangu." Demeke alinena.

16

Demeke alichukua kisu chake. "Nitakujengea chumba kipya! Naomba msamaha kwa kukiteketeza chumba chako cha kwanza," Meseret alisema.

"Sitaki chumba kipya. Ninataka mbaazi zangu," Demeke alimjibu. Alianza kukitia kisu chake makali. "La! La! Tafadhali, ngoja! Hebu twende tukawaone wazee. Tafadhali rafiki yangu wa jadi, wacha wazee waamue." Meseret alilia.

17

Meseret na Demeke walienda kuwaona wazee wa kijiji. Wazee waliongea kwa muda mrefu.

Mwishowe walimwambia Meseret, "Ulikosea ulipokataa kumlipa Demeke nusu ya punda wake. Ulikosea pia ulipokiteketeza chumba chake, na wanao walipozila mbaazi zake."

18

Wazee walimgeukia Demeke wakasema, "Unataka kuwaua wanawe Meseret. Hilo ni kosa pia. Huu ni uamuzi wetu. Lazima Meseret ampatie Demeke nusu ya miti yake yote, mashamba, ng'ombe na kondoo. Hivyo, mtaishi pamoja kwa amani."

19

Meseret alimpatia Demeke nusu ya mali yake.

Waliishi pamoja kwa furaha bila kugombana tena.

20
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Hakimu asiyekuwa na busara
Author - Magabi Eynew Gessesse, Elizabeth Laird
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Brian Wambi
Language - Kiswahili
Level - Read aloud