Fisi na Kobe
Alice Mulwa
Salim Kasamba

Fisi mlafi aliishi katika kijiji cha Mkosi.

1

Katika kijiji jirani, aliishi Kobe mwoga.

Fisi na Kobe walikuwa marafiki.

2

Fisi alisikia kwamba kulikuwa na nyuki waliotengeneza asali tamu kuliko yote. Nyuki hao walisafiri mbali na mizinga yao mara moja kwa mwaka.

"Lazima tuipate ile asali nyuki watakapokuwa safarini," Fisi alimwambia Kobe.

3

Ingawa Kobe aliogopa kwenda, hakuwa na ujasiri wa kukataa.

Asubuhi iliyofuata, Fisi na Kobe walianza safari yao. Fisi alienda kwa kasi huku Kobe akijikokota nyuma kwa woga.

4

Walipanda milima wakashuka kisha wakavuka mabonde.

Waliuvuka mto mkubwa wakaendelea na safari yao wakiwa na nia ya kuifikia ile mizinga ya nyuki.

5

Hatimaye, waliona mizinga ya nyuki milimani kwenye miti. Fisi alikwenda kwa haraka.

Kobe alikuwa tayari kuzirai kutokana na njaa na uchovu.

6

Fisi alipoufikia mzinga mkubwa zaidi, alimwambia Kobe, "Haraka! Panda juu ya mti uuangushe mzinga chini."

7

Kobe aling'ang'ana kuupanda mti. Alipofanya hivyo, aliangalia chini mara kwa mara asije akaanguka.

Fisi alikasirishwa na kitendo hicho akaanza kumpigia Kobe kelele.

8

Kobe alipougusa mzinga, alisikia sauti ya nyuki. Kumbe walikuwa bado ndani ya mzinga wao!

Kobe alishtuka akaanguka chini.

9

Mzinga wa nyuki ulimwangukia Kobe akafunikwa na kufichwa na asali!

Fisi alianza kuilamba ile asali. Lakini nyuki hawakufurahia kitendo hicho.

10

Nyuki walimuuma Fisi kila sehemu ya mwili akaamua kukimbilia usalama wake.

Hata hivyo, nyuki walimfuata wakaendelea kumuuma.

11

Fisi aliteremka kutoka mlimani, akavuka mto na bonde.

Nyuki waliendelea kumuuma wakati huo wote.

12

Kobe naye alikuwa bado chini ya mzinga mkubwa. Hatimaye, kila kitu kilikuwa kimya.

Kobe aligundua kuwa mzinga na asali vilikuwa vimekaukia mgongoni kwake.

13

Kobe alitambua kuwa hakuhitaji tena kujificha kichakani.

Gamba jipya alilopata lingeweza kumkinga na hatari yoyote.

14

Fisi alikuwa amechoka na alijaa vidonda mwilini. Alizirai kabla kufika nyumbani.

Alipoamka, aligundua kwamba mishale ya nyuki ilisababisha madoadoa kwenye ngozi yake.

15

Hivi ndivyo kobe alivyopata gamba lake ngumu naye fisi akapata madoadoa kwenye ngozi yake.

Urafiki kati ya fisi na kobe uliisha.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Fisi na Kobe
Author - Alice Mulwa
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Salim Kasamba
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs