Hapo zamani, wanyama hawakuwa na miguu.
Wote walitambaa.
Watu pekee ndio waliotembea.
Walikuwa wamepatiwa miguu na Maguru.
Siku moja, Maguru aliamua kuwapatia pia wanyama miguu.
Alitaka watembee kama vile binadamu. Kwa hivyo aliwatangazia!
Wanyama walifurahi. Sasa wangeweza kutembea na kukimbia.
Waliimba na kucheza.
Ilikuwa vigumu kutambaa. Tumbo zao zilikwaruzwa.
Wangepata miguu wangeweza pia kusimama na kuona mbali.
Siku ilipofika, wanyama wengi walitambaa kwenda kwa Maguru.
Kila mnyama alipata miguu minne.
Kila ndege alipata miguu miwili.
Walifanana tofauti waliposimama.
Baadhi yao walianguka waliposimama.
Walizunguka kijijini wakiwaambia watu, "Hatutatambaa tena."
Wa mwisho kwenda kwa Maguru alikuwa Jongoo.
Maguru alimwuliza, "Kuna mwingine nyuma yako?"
Jongoo alijibu, "La! Mimi ndiye wa mwisho."
Maguru aliwaza, "Ikiwa yeye ndiye wa mwisho, nitaifanyia nini miguu itakayobaki?"
Maguru aliamua kumpatia Jongoo miguu yote iliyokuwa imebaki.
Jongoo aliondoka kwa furaha akiwa na miguu mingi.
Aliwaza, "Nitaweza kwenda kwa kasi kuwaliko wote."
Baada ya Jongoo kuondoka, Nyoka alifika.
"Tafadhali, nipatie nami miguu," alimsihi Maguru.
"Nimepatiana miguu yote kwa waliotangulia. Wewe ulikuwa wapi?" Maguru alimwuliza.
Nyoka alimjibu, "Nililala kupita kiasi."
Maguru alitafuta kila mahali lakini hakupata miguu yoyote ya kumpatia Nyoka.
Maguru alimwambia, "Hakuna miguu iliyobaki." Nyoka alitambaa akarudi bila miguu.
Hiyo ndiyo sababu nyoka huwa hawalali. Wanasubiri kupata miguu.