Likizo kwa Bibi
Violet Otieno
Catherine Groenewald

Odongo na Apiyo waliishi na baba yao mjini.

Kila wakati waliitazamia likizo si tu kwa shule kufungwa, bali pia kumtembelea bibi yao.

Bibi aliishi katika kijiji cha wavuvi karibu na ziwa kubwa.

1

Odongo na Apiyo walifurahi kwani ulikuwa wakati wa kumtembelea bibi kwa mara nyingine.

Usiku huo, walifunganya mifuko yao tayari kwa safari ndefu ya kwenda kijijini.

Usiku kucha waliongea juu ya likizo na kumtembelea bibi kijijini.

2

Asubuhi iliyofuata, waliondoka mapema kwenye gari la baba yao kuelekea kijijini.

Safarini, waliiona milima, wanyama wa pori na mashamba ya majani chai.

Walihesabu magari yaliyopita na kuimba nyimbo walizofunzwa shuleni.

3

Baada ya muda, walilala kwa sababu ya uchovu.

4

Walipofika kijijini, baba aliwaamsha.

Walimkuta bibi akipumzika kwenye mkeka chini ya mti.

Bibi alikuwa mwanamke mrembo na mwenye nguvu.

5

Bibi aliwakaribisha kwa kucheza na kuimba kwa furaha.

Wajukuu wake walifurahi na kumpa zawadi walizomletea kutoka mjini.

"Fungua zawadi yangu kwanza," Odongo alimsihi. "La, atafungua yangu kwanza!" Apiyo akasema.

6

Bibi aliwabariki wajukuu wake baada ya kuzifungua zawadi.

Alipendezwa na zawadi walizompelekea.

7

Baada ya kupmzika, Odongo na Apiyo walitoka nje.

Walifurahia kucheza na vipepeo na ndege.

Hawakuweza kuwaona vipepeo na ndege wengi mjini.

8

Walipanda mitini na kuchezea ziwani.

9

Giza lilipoanza kuingia, walirejea nyumbani.

Bibi aliwaandalia chakula, lakini walilala kabla ya kumaliza kukila!

10

Siku iliyofuata, baba yao aliondoka na kurudi mjini.

Aliwaacha Odongo na Apiyo nyumbani kwa bibi.

11

Odongo na Apiyo walimsaidia bibi yao kufanya kazi za nyumbani.

Walitafuta kuni na kuchota maji.

Wakakusanya mayai na kuchuna mboga kutoka kwenye bustani.

12

Bibi aliwafunza wajukuu wake jinsi ya kupika ugali mwororo walioula kwa kitoweo cha nyama.

Pia, aliwaonyesha namna ya kupika wali wa nazi walioula kwa mchuzi wa samaki.

13

Siku moja subuhi, Odongo aliwapeleka ng'ombe wa bibiye malishoni.

Kwa bahati mbaya, waliingia shambani mwa jirani.
Jirani alitishia kuwafungia ng'ombe kwake kwa kuila mimea yake.

Baada ya siku hiyo, Odongo alikuwa mwangalifu zaidi.

14

Siku ya soko, Odongo na Apiyo walienda pamoja na bibi. Bibi alikuwa na kibanda cha kuuzia mboga, sukari na sabuni.

Apiyo aliwaelezea wateja bei za bidhaa. Odongo naye aliwapakia wateja bidhaa walizonunua.

15

Kabla ya kurejea nyumbani walimsaidia bibi kuhesabu pesa alizopata siku hiyo.

Baadaye, walikunywa chai pamoja.

16

Likizo ilipokaribia kuisha, watoto walilazimika kurudi mjini.

Bibi alimpatia Odongo kofia naye Apiyo akampatia sweta kama zawadi.

Aliwatayarishia chakula watakachokula safarini.

17

Baba yao alipofika, hawakutaka kuondoka. Walimsihi Bibi kwenda nao mjini.

Lakini, alitabasamu na kusema, "Nina kazi nyingi shambani, siwezi kwenda mjini. Nitawasubiri mje hapa kijijini tena."

18

Odongo na Apiyo walimkumbatia na kumuaga.

19

Odongo na Apiyo waliwaambia marafiki zao kuhusu maisha kijijini.

Baadhi yao waliamini kuwa maisha ya mjini ni bora. Bali wengine waliamini maisha ya kijijini ni bora zaidi.

Lakini wote walikubali kwamba Odongo na Apiyo walipendwa na bibi yao.

20
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Likizo kwa Bibi
Author - Violet Otieno
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Catherine Groenewald
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs