Basi kubwa la bluu
Mecelin Kakoro
Mango Tree

Kulikuwa na basi moja tu katika kijiji cha akina Ebei.

Lilikuwa basi kubwa lenye rangi ya bluu. Lilinguruma sana.

1

Siku moja mamake Ebei alisema, "Kesho tutaenda mjini kununua sare yako ya shule."

2

Ebei alifurahi sana. Kumbe atasafiri katika lile basi kubwa la bluu!

Usiku huo hakupata lepe la usingizi.

3

Mamake alipoenda kumuamsha, Ebei alikuwa tayari amevaa.

4

Ebei na mamake walienda kwenye kituo cha basi.

Walisubiri lile basi kubwa la bluu. Basi halikufika.

5

Watu wengine walifika pale kituoni. Wote walilalamika kuwa basi lilichelewa.

Mmoja aliuliza, "Basi limetuacha?"

6

Ebei alikuwa na wasiswasi. "Tusipokwenda mjini, sitapata sare yangu ya shule," aliwaza.

7

Baadhi yao walikata tamaa wakarudi nyumbani.

Ebei alilia akakataa kurudi. "Tutasubiri zaidi," mamake alimtuliza.

8

Ghafla, walisikia mngurumo. Wakaona vumbi hewani.

Basi lilikuwa linakuja kwa kasi.

9

Basi halikuwa la bluu wala halikuwa kubwa. Basi lile lilikuwa dogo na jekundu.

Waliosubiri waliliangalia tu na hawakuingia ndani.

10

Dereva aliwaita, "Ingieni! Ingieni! 
Tumechelewa sana leo."

11

Ebei na mamake walikuwa wa kwanza kuingia.

Mara wote waliingia ndani ya basi lile dogo jekundu.

12

Ebei alichungulia dirishani.

Aliwaona watu wengi zaidi wakiingia ndani ya basi.

13

Mara basi likaondoka. Ebei aliwaona watu wengine wakikimbia kulifikia basi.

Walikuwa tayari wamechelewa.

14

Mamake Ebei alimwuliza dereva, "Liko wapi basi kubwa la bluu?" 

Dereva alimjibu, "Basi la bluu liliharibika. 
Linatengenezwa, kesho litakuja."

15

Ebei hakujali rangi wala ukubwa wa basi.

Alifurahi kuwa basi lile lilikuwa linawapeleka mjini. Hatimaye, atanunuliwa sare ya shule.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Basi kubwa la bluu
Author - Mecelin Kakoro
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Mango Tree
Language - Kiswahili
Level - First sentences