Sungura chini ya mti
Phumy Zikode
Wiehan de Jager

Sungura alikuwa amelala chini ya mtofaa.

Tofaa lilianguka chini kutoka tawi moja.

1

Sungura aliisikia sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura, kimbia!'

Sungura aliamka, na bila kukawia, akaanza kukimbia mbio sana.

2

Sungura alikutana na Kuku. "Mbona unakimbia?" Kuku alimwuliza.

Sungura akamjibu, "Sijui. Nilisikia tu kitu kikianguka nayo sauti ikasema, 'Kimbia, Sungura kimbia!'"

3

Kuku alishituka akaanza kukimbia aliposikia maneno aliyosema Sungura.

4

Walikutana na Mbwa akawauliza, "Kwa nini mnakimbia?"

Kuku akamjibu, "Sijui. Nilisikia Sungura akipiga makelele naye hajui. Alisikia kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura kimbia!'"

5

Mbwa akashangaa akaanza kukimbia pamoja na Sungura na Kuku.

6

Walikutana na Farasi akawauliza, "Mbona mnakimbia?"

Mbwa akamjibu, "Sijui. Nilisikia Kuku akisema hajui na wala Sungura hajui. Sungura alisikia kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura kimbia!'"

7

Farasi naye akaanza kukimbia pamoja na Sungura, Mbwa na Kuku.

8

Walikutana na Punda akawauliza, "Kwa nini mnakimbia?"

Farasi alimjibu, "Sijui. Nilimsikia Mbwa akisema hajui. Yeye alimsikia Kuku ambaye hajui. Kuku naye alimsikia Sungura ambaye pia hajui. Sungura alisikia tu kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura, kimbia!'"

9

Basi Punda pia akaanza kukimbia pamoja na Sungura, Mbwa, Kuku na Farasi.

10

Walikutana na Ng'ombe akawauliza, "Kwa nini mnakimbia?"

Punda alimjibu, "Sijui. Nilisikia alivyosema Farasi, naye hajui. Yeye alisikia Mbwa na Mbwa hajui. Alimsikia Kuku naye Kuku hajui. Alimsikia Sungura naye pia hajui. Sungura alisikia kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura, kimbia!'"

11

Ng'ombe akapata wasiwasi na akaanza kukimbia pamoja na Sungura, Mbwa, Kuku, Farasi na Punda.

12

Walikutana na Paka akawauliza, "Kwa nini mnakimbia?"

Ng'ombe alijibu, "Sijui. Nilisikia tu alivyosema Punda naye hajui. Yeye alimsikia Farasi naye Farasi hajui. Alimsikia Mbwa ambaye hajui. Yeye alimsikia Kuku na Kuku hajui. Kuku alimsikia Sungura ambaye hajui ila alisikia kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura, kimbia!'"

13

Paka naye akaanza kukimbia pamoja na wanyama wengine.

14

Walikutana na mvulana aliyekuwa amepanda baiskeli. Mvulana aliwauliza, "Mbona nyote mnakimbia?"

Wanyama walimjibu, "Hatujui. Tulimsikia Sungura alivyosema naye hajui. Alisikia kitu kikianguka na sauti ikisema, 'Kimbia, Sungura, kimbia!'"

15

Mvulana yule aliangua kicheko akasema, "Upepo uliangusha tofaa. Mimi ndiye nilisema, 'Kimbia, Sungura kimbia!'"

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Sungura chini ya mti
Author - Phumy Zikode
Translation - Pete Mhunzi
Illustration - Wiehan de Jager
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs