

Akai alipokuwa mdogo, mamake alikuwa na mazoea ya kumlaza kwenye mkeka maridadi.
Mkeka huo ulitengezwa na shangaziye Akai kwa majani ya mtende.
Mkeka wa Akai ulikuwa na rangi za waridi, bluu na kijani kibichi.
Ulikuwa tofauti na mikeka mingine aliyokuwa nayo mamake.
Makazi ya kina Akai yalikuwa katika sehemu kavu, iliyojaa mawe na yenye joto.
Kulikuwa na nge, buibui na nyoka pia.
Akai hakuwahi kuumwa na viumbe hao hatari.
"Huu mkeka wako wa kipekee hukukinga na hatari." Mamake alimwambia.
Akai alikuwa mtoto mwerevu.
Alijua mahali kilipokuwa kisima cha karibu.
Vile vile alijua mahali ilipokuwa manyatta ya nyanyake.
Mara kwa mara alienda kwa nyanyake kunywa maziwa ya ngamia.
Siku moja, Akai aliondoka nyumbani kwenda kwa nyanyake.
Alipotelea milimani, akaogopa.
Aliamua kuketi chini ya mti wa edome kusubiri usaidizi.
Muda mfupi baadaye, alilala akaota ndoto.
Ndotoni, Akai alikuwa amelala kwenye mkeka wake kipekee. Bi kizee aliyefanana na nyanyake alikuwa akimchunga.
Bi kizee huyo alitabasamu na kumpa maziwa. Akai alipounyoosha mkono wake kuyapokea, aliamka.
Akai aliyafungua macho yake pole pole.
Alitazama juu akamwona ndege mdogo wa rangi ya bluu kwenye tawi.
Akai aliposimama, yule ndege alipapatisha mbawa zake kisha akamwongoza.
Akai alimfuata.
Akai alifika mahali penye njia panda.
Yule ndege akakitupa kipande cha mkeka kilichofanana na ule wake.
Akai alikichukua kipande hicho akakitazama kwa makini.
Aliziona nyayo alizozifahamu kuwa za mamake.
Baadaye, alikiona kisima walikochota maji.
Akai hatimaye alifika nyumbani. Watu wote wa familia yake waliimba na kucheza kumkaribisha nyumbani.
Walimchinjia mbuzi, wakachoma nyama na kusherehekea kurudi salama kwa mtoto wao.
Akai aliukalia mkeka wake wa kipekee akila kipande kikubwa cha nyama.
Akai alifurahi sana.

