

Safari yetu ilianza alasiri. Tulipanda gari moshi saa tisa kwenda mji wa kitalii wa Voi, Kaunti ya Taita Taveta.
Kituo cha gari moshi kilipendeza na kilikuwa na mikahawa kadhaa ambapo tulipata vitafunio.
Kulikuwa pia na ukumbi mkubwa ambamo wote tuliketi na kujipumzisha.
Gari moshi lilivuka mandhari ya kupendeza ya mbuga ya kitaifa ya Tsavo. Tuliona ngiri, paa, dik dik, kanga, nyani, pundamilia na kikundi cha mbwa mwitu.
Ilitusisimua sana. Tulijua kwamba kulikuwa na mengi zaidi tutakayoona tulipokuwa tukitulia kwenye hoteli huo usiku.
Tuliraukia mandhari yaliyopendeza ya milima iliyozingira mji. Gari la kutalii lilituchukua kutoka kwenye hoteli yetu na tukaondoka.
Tuliweza hata kuona mlima wa Kilimanjaro tulivyoanza kuingia kwenye nyika iliyokauka na kua na vumbi.
Kwanza, tuliwasili kwenye uwanja uliokuwa wazi ambapo tulimuona kifaru akiwa pekee yake.
Tulipomsongelea, alitahadhari, akatuangalia kwa umakini. Kisha, polepole, aligeuka na kuanza kutembea akielekea kwenye dimbwi lililojaa tope.
Kiongozi wetu alituelezea kuwa vifaru wanapenda kijipaka matope. Hiyo inaondoa wadudu kwenye ngozi zao. Pia inawakinga kutokana na joto la jua na kuwaweka baridi.
Kifaru huyo mkubwa aliingia mzima kwenye kidimbwi hicho cha tope na kuzama ndani polepole. Ilionekana kumridhisha sana.
Tuliendelea, tukakutana na wanyama mbalimbali wadogo. Kisha, kulikuwa na kundi kubwa la nyati.
Ndama wa hao nyati walisimama chini ya mama zao. Kiongozi wetu akatuambia kua hiyo ndiyo njia yao ya kujikinga kutokana na jua na pia kujificha ili wasionekane na wawindaji.
Nyati hao walikuwa wanakula nyasi iliyopendeza ya hudhurungi. Walitafuna kwa uvivu kwa kile kilichoonekana kama mwendo wa polepole sana.
Walionekana kuburudika sana. Pembe za nyati zinaweza kuwa na upana kadri ya urefu wa mtu mzima.
Mngurumo mkubwa ulisikika. Ghafla, fujo ikazuka kwenye kikundi. Ng'ambo nyingine, tukaona vumbi na wanyama wakikimbilia kila upande.
Ilikuwa taswira ya kuvutia! Simba dume mkubwa alimrukia nyumbu. Kiongozi wetu alituambia kuwa tulichoshuhudia ni nadra sana kwani ni simba jike ndio huwinda kwa niaba ya kikundi.
Shirika la huduma ya wanyamapori lilikuwa linafanya sensa ya wanyama wote. Helikopta za kijani zilipita angani zikiwa zimebeba walinzi pori na wanasayansi wakikusanya data.
Sensa inafanyika baada ya kila miaka mitatu ili kudhibitisha idadi ya wanyamapori.
Simba aliburuta mzoga chini ya mti wa acacia.
Chui aliketi kwa tawi la mti bila kuonekana rahisi. Alitazama kwa macho ya kutisha.
"Chui ni mwindaji wa faragha na akikutana na wenzake lazima kuwe na vita," kiongozi wetu alisema.
Ilikuwa alasiri na wanyama wengi walikusanyika karibu na vidimbwi vya maji ili kukata kiu na kucheza.
Ndovu wakubwa walikunywa maji na kujinyunyizia mengine ili kuondoa joto mwilini. Walipendeza sana.
Tulimaliza zaidi ya saa moja tukiwaangalia bila hata kuchoka.
Jua lilikuwa linatua nyuma ya milima tulipokuwa tukielekea kwenye lango la mbuga ili tufike kabla ya giza kuingia. Wageni hawaruhusiwi ndani ya mbuga usiku.
Tuliwaacha wanyama nyuma. Ilikuwa siku ya kupendeza sana!
Upesi tulikuwa tushafika kwenye lango la mbuga la Sala, lililo karibu na mji wa pwani wa Malindi.
Tulikuwa tumepanga kulala Malindi kabla ya kusafiri kurudi nyumbani.
1. Taja wanyama wnaojulikana kama Watano Wakubwa.
2. Taja mbuga zilizomo nchini kwenu.
3. Mnyama yupi unayempenda zaidi?
4. Je, sensa ni nini?
5. Mbona wageni hawaruhusiwi mbugani usiku?

