

Naka na Nala wanafanya kazi katika bustani yao. Wanapanda mboga.
"Kwa nini tunafanya kazi kwa bidii kwenye jua?" Nala anashusha pumzi.
"Tunafanya kazi kwa bidii kwa sababu tunapenda dunia yetu!" Naka anasema.
"Tukitunza dunia, dunia itatutunza sisi," anaongezea.
"Tunapanda mboga ili tuweze kula vyakula vyenye afya," Naka anasema.
"Kupanda mboga zetu wenyewe kunaweza pia kutuokolea pesa," Nala anaongeza.
"Ulikuwa ukisema nini kuhusu dunia? Niambie Zaidi?" Nala anauliza.
Naka anasema, "Hebu tuketi, na nitakuambia mengi kuhusu dunia yetu."
Naka anaanza, "Dunia ni sayari ya duara tunamoishi.
Takriban watu bilioni nane wanaishi hapa! Dunia inazunguka jua."
"Dunia imeundwa kwa ardhi, hewa, na maji.
Sayari yetu inachemka ndani kwa joto. Viumbe hai huishi juu ya dunia," Naka anaeleza.
Nala anakatiza, "Kwa nini tusianguke kutoka duniani?"
"Nguvu ya mvuto inatushikilia hapa. Nguvu hii hutuvuta kuelekea kwenye sayari," Naka anajibu.
"Tunawezaje kutunza dunia?" Nala anauliza.
Naka anamjibu, "Tusiichafue dunia. Tunapaswa kuchakata na kupunguza taka zetu."
Naka anaendelea, "Tuchakate plastiki, karatasi, glasi na makopo.
Inawezekana kutengeneza vitu vipya kutoka kwa nyenzo zilizochakatwa. Tunatupa vitu vingi sana."
Naka anatamatisha, "Lazima tutunze dunia kwa sababu binadamu wanaihitaji kuwa hai."
Nala atangaza, "Tunafaa kurudi kazini!"
Maswali
1. Nala na Naka wafanya nini? Kwa nini?
2. Andika mambo 4 ya kweli kuhusu sayari yetu.
3. Kwa nini tunafaa kuitunza dunia?
4. 'Kuchakata' vitu ina maana gani?
5. Nini kinaweza kuchakatwa? Orodhesha mifano.
6. Nini lingine tunaweza kufanya kulinda dunia?


