Tunaishi katika kiota
Nina Orange
Kenneth Boyowa Okitikpi

Wadudu huishi katika nyumba tofauti. Baadhi ya wadudu huishi pamoja katika makundi makubwa na wengine huishi peke yao.

Kitabu hiki kinauhusu Naeku na Naserian - mchwa wawili ambao ni dada wanaoishi katika nyancha za kusini mwa Kenya.

Dada hao wanaishi katika koloni pamoja na takriban mchwa wengine 80,000.

1

Koloni ya mchwa huishi katika kiota ambacho hutengenezwa kwa udongo. Kiota hiki kinaweza kuwa chini ya ardhi, juu ya ardhi, au pote pawili.

Sehemu ya kiota tunayoweza kuiona juu ya ardhi ni kilele. Kilele hiki kina urefu wa kati ya mita mbili hadi mita tano juu ya ardhi.

2

Mchwa katika koloni hufanyia kikundi kizima shughuli tofauti. Naeku na Naserian ni mchwa wafanyakazi. Mchwa wote wafanyakazi ni wa kike. "Sisi ndio wajenzi na wahandisi!" Naeku anasema.

Mchwa wafanyakazi hujenga na kudumisha kiota cha mchwa. Naserian anasema, "Tunajenga miundo mikubwa iliyo tata."

3

"Hebu tueleze jinsi tunavyojenga nyumba zetu," Naeku anapendekeza. ''Tunaanza kwa kuchimba vichuguu ndani ya ardhi."

Naeku anakatiza, "Tunatumia taya zetu zenye nguvu kuchimba ardhini. Tunaweza kuhamisha udongo mwingi sana!''

4

"Ili kuhakikisha kuwa kuta za vichuguu hivyo ni imara, tunavifunika kwa mchanganyiko wa mate na udongo unaoshikamana," Naserian anasema.

"Mchanganyiko wa mate unapokauka, unakuwa mgumu kama udongo. Makazi ya mchwa yanaweza kudumu kwa muda mrefu sana," Naeku anaongeza.

5

"Tunatoa udongo tunaochimba na kutumia kujenga kilima juu ya ardhi. Kilima kawaida ni umbo la mviringo au umbo la koni, lenye vichuguu vingi," anasema Naserian.

"Baadhi ya vilima vya mchwa vinaweza kuwa na urefu wa mita tisa!" anasema Naeku.

6

Mchwa ni wadudu wa kijamii wanaoishi katika kikundi kikubwa. Wana majukumu tofauti katika kuunda na kudumisha koloni.

Mchwa wafanyakazi kama Naserian na Naeku huchimba na kujenga viota. Mchwa wanajeshi hulinda kiota.

Wafanyakazi na wanajeshi huenda nje kutafuta maeneo mapya ya kujenga viota.

7

Mchwa wauguzi wanatunza malkia na mchwa wachanga wanaoitwa viluwiluwi.

Kiota kina sehemu tofauti. Kuna vyumba vya malkia, vyumba vya viluwiluwi, na vyumba vya kuhifadhi chakula. Vichuguu vinaunganisha maeneo tofauti.

Malkia ndiye mchwa mkubwa zaidi na anaweza kuishi kwa muda mrefu zaidi.

8

Naserian anaendelea, "Tunajenga vichuguu au mashimo kwenda juu ili hewa safi iweze kupita ndani ya kiota."

Naeku anaongeza, "Mchwa wanahitaji hewa safi ili waishi." Naserian anaeleza, "Vichuguu au mashimo pia husaidia kudhibiti joto katika kiota ili kisiwe moto sana."

9

"Tuna bustani katika kiota chetu ambapo tunapanda uyoga. Tunakusanya vipande vidogo vya mimea na vifaa vingine vya asili, ambavyo tunatumia kukuza uyoga," anasema Naserian.

"Vizuri sana!" anashangaa Naeku. "Bustani za uyoga hulisha koloni nzima. Sisi ndio aina pekee ya mchwa wanaolima uyoga."

10

Koloni ya mchwa ina malkia na mfalme. Wafanyakazi hulisha na kulinda wanajamii hawa muhimu wa koloni.

Mchwa malkia kawaida huishi kwa kati ya miaka 20 hadi 30. Anaweza kutaga mamilioni ya mayai katika maisha yake.

Viluwiluwi huanguliwa kutoka kwenye mayai na kutunzwa na mchwa wauguzi.

11

Naserian anasema, "Jamii ya mchwa ina mpangilio mzuri sana. Kila mchwa huchangia uhai wa koloni nzima na ukuaji wake."

Naeku anaongeza, "Kila mmoja wetu ana kazi ya kufanya, na tunafanya. Mchwa hufanya kazi pamoja vizuri sana."

"Ndio," Naserian anakubaliana naye. "Sasa, hebu turudie ile kazi ya kuchimba!''

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Tunaishi katika kiota
Author - Nina Orange, Ursula Nafula
Translation - Anne Kamau
Illustration - Kenneth Boyowa Okitikpi
Language - Kiswahili
Level - Read aloud