

Watu wanaishi katika nyumba aina tofauti. Baadhi ya watu wanaishi katika nyumba zilizojengwa kudumu kwa muda mrefu. Wengine wanaishi katika nyumba za muda ambazo hazidumu kwa muda mrefu.
Kitabu hiki kinahusu makazi ya muda yanayoitwa manyata, ambayo yanajumuisha vyumba vya kitamaduni.
Manyatta hii ipo kaskazini ya kati ya Kenya, katika Kaunti ya Samburu. Sidai na Naeku ambao ni dada, wanashiriki chumba kimoja, na wazazi wao na kaka yao mdogo wanashiriki kingine.
Mjomba wao na kaka zao watatu wakubwa wanakaa kwenye vyumba vingine, pamoja na familia zao.
Familia hizi hulisha mifugo wao pamoja na kusaidiana. Hawakai sehemu moja kwa muda mrefu. Wanahama hama kutafuta maeneo mapya ya malisho ya mifugo wao.
Kando ya manyatta kuna uzio wa matawi ya miiba. Uzio huu unawazuia mifugo wasitoke nje na watu wasiojulikana kuingia ndani.
"Tunaanza mchakato wa ujenzi kwa kukusanya vifaa kutoka kwenye mazingira yetu. Tunakusanya matawi ya miti ya kujenga muundo wa msingi wa chumba," Sidai anasema.
Naeku anaongeza, "Tunajua jinsi ya kutumia vifaa vya asili kujenga nyumba zetu. Kila mtu katika manyatta anasaidia katika ujenzi."
Tunatumia matawi makubwa kutengeneza fremu imara ya kuta. Tunafunga fremu ya paa kwenye fremu ya kuta kwa kutumia mizizi, na hivyo kutengeneza fremu thabiti kwa chumba chote," Sidai anaelezea.
"Vyumba vina paa za chini, na hivyo ni vigumu kwa upepo kuvipindua," Naeku anaongeza.
Sidai anaendelea, "Mara tu fremu ya chumba inapokuwa imesimama, tunashonea matawi membamba kati ya matawi makubwa."
Naeku anaongeza, "Tunatengeneza tabaka nene za nyasi na kuzifunga kwenye fremu ya paa. Hii inaitwa kuezeka." "Kuezeka vizuri kunatulinda kutokana na mvua na jua," anaongeza Sidai.
Sidai anaongeza, "Paa za vyumba vyetu zinaweza nyooka au kuwa mviringo."
Naeku anasema, "Kupaka tope ni sehemu ya ujenzi ninayopenda zaidi. Tunachanganya matope na samadi ya ng'ombe kutengeneza plasta. Tunapaka plasta hii kwenye fremu ya kuta, tukijaza nafasi zilizopo. Hii huzuia upepo na mchanga kuingia."
Sidai anaendelea, "Kupaka plasta kwenye kuta kunaziba kuta hizo mara tu zinapokauka. Pia tunapaka plasta juu ya kuta. Plasta iliyokauka ni ngumu na imara."
Naeku anaongeza, "Hakuna madirisha kwenye kuta, lakini chumba chetu kina mlango wa mbao."
"Upakaji wa plasta kwenye kuta husaidia kuhifadhi joto chumbani," anasema Sidai. "'Kuhifadhi joto' linamaanisha nini?" anauliza Naeku.
"Kuta za matope na samadi husaidia kuweka chumba kuwa baridi ndani wakati nje kuna joto. Katika msimu wa baridi, kuta zinasaidia kutuweka joto ndani kwa kuhifadhi joto la moto," anajibu dada yake.
"Watu wote katika manyatta wanashiriki katika ujenzi, na sote tunasaidia kuvunja vyumba tunapohama.
Sio vigumu kuvunja miundo na kutumia sehemu hizo tena mahali pengine," Sidai anaeleza.
"Vifaa vyetu vya ujenzi ni vyepesi, kwa hivyo ni rahisi kuvibeba. Tunatumia ngamia au punda kubeba vifaa vyote muhimu kutoka manyatta yetu ya zamani. Kwa mfano, paa lenye nyasi," anasema Sidai.
"Pia tunaweza kukusanya vifaa vingi zaidi vya ujenzi kutoka kwenye mazingira mapya," anaongeza Naeku.
"Nyumba yetu inatufaa tunavyoishi, ambayo ni kuhama hama na mifugo yetu," anasema Sidai.
"Kuhama hama kunamaanisha hatuwezi kwenda shule na marafiki zetu daima," anasema Naeku.
"Shule yetu inaturuhusu kuomba vitabu, na tunajaribu kufuatilia masomo yetu," anamalizia Sidai.

