

Hapo zamani za kale, kwenye shamba ndogo karibu na kijiji kidogo.
Aliishi kuku mdogo aliyeitwa Daisy.
"Ningependa kuruka juu, juu angani, nitakapokua mkubwa," Daisy alisema.
Lakini kuku wengine wote walimcheka.
"Wewe ni wa ajabu sana," walisema. "Hatutacheza nawe tena."
"Daisy, sote tunaweza kupapata mabawa yetu lakini ni vigumu sana kwa kuku kuruka," Mama alimwambia.
Daisy hakutaka kukata tamaa. Kila siku alifanya mazoezi peke yake, akipapata mabawa yake.
Papata, papata, papata, angepapata mabawa yake lakini hakuweza kunyanyuka kutoka chini.
Alipofanya mazoezi, alijiona ameruka juu na kuwatazama kuku wengine chini.
Alijiwazia akiwa ameruka na kuwapita shomoro na mbayuwayu. "Waa!" Ndege wangesema. "Kuku anayeweza kuruka!"
Kwa hivyo papata, papata, papata, kila siku Daisy angepapata mabawa yake.
Angeweza kunyanyuka kutoka chini lakini angeanguka chini tena.
"Sitawahi kuruka!" Daisy alimlilia Mama. "Ni kweli wengine wanavyosema kuwa sitawahi."
"Daisy, wewe ni tofauti na kuku wengine. Wao hawataki kuruka lakini wewe unataka! Unaweza kufanya hivyo," Mama alisema.
Siku iliyofuata Daisy alipanda juu ya kibanda cha kuku na papapta, papata, papata, akapapata mabawa yake.
Aliruka angani na kupapata mabawa yake na kupapata mabawa yake na kupapata mabawa yake na ...
BAM! Alianguka kwa kishindo!
Kuku wengine wakacheka kwa sauti.
"Ha ha ha! Tulikuambia! Kuku hawawezi kuruka!"
Lakini siku iliyofuata, Daisy alipanda juu zaidi, hadi juu ya chumba.
Papata, papata, papata, Daisy alipapata mabawa yake.
Aliruka angani na kupapata mabawa yake na kupapata mabawa yake na kupapata mabawa yake na ...
Aliendelea kuruka! Upepo uliokuwa chini ya mabawa yake ulizidisha nguvu na akaruka juu zaidi!
Shomoro na mbayuwayu walisema, "Ajabu! Kuku anayeruka!"
Na kuku wengine walitaka kuwa kama yeye.
Wakasema, "Oo Daisy, wewe ni wa ajabu!"


