

Hapo zamani, katika jiji kubwa la Johannesburg, mtoto msichana alizaliwa. Mtoto huyo alikuwa mimi.
Mama yangu alinitaja Miriam. Miriam Makeba.
Mama alikuwa mganga wa kienyeji, lakini pia aliwasafishia watu wengine nyumba zao.
Ilikuwa vigumu kwa mama kupata pesa za kututosha sisi wawili. Alianza kuuza pombe ya kienyeji ili kupata pesa zaidi.
Sheria za nchi hiyo zilisema kwamba kuuza pombe ya kienyeji ilikuwa mbaya. Polisi walimpeleka mama jela kwa muda wa miezi sita.
Nilikuwa na umri wa siku 18 tu, na nilimhitaji mama yangu. Kwa hivyo ingawa nilikuwa mtoto mchanga, nilienda gerezani pia.
Nikiwa msichana mdogo nilipenda kuimba. Nilipokua mkubwa, nilimsaidia mama kusafisha nyumba. Nilipoimba nikifanya kazi, kazi ilikwenda haraka na siku zilionekana kung'aa. Kuimba kulinifurahisha kuliko ninavyoweza kuelezea.
Niliimba kanisani na hii ilifurahisha wengine pia. Muziki una uwezo wa kuwaleta watu pamoja.
Tulipokuwa tukiimba, tulikuwa jasiri na wenye nguvu.
Watu walisema sauti yangu ilikuwa zawadi na nyimbo zangu zilikuwa za kipekee.
Niliimba na wanamuziki wengine na muziki wetu ulisikika ulimwenguni kote.
Nyumbani ilikuwa Sophiatown, mahali pa utamaduni na muziki. Sophiatown, mahali ambapo watu wa Afrika Kusini wangeweza kutunga muziki kwa maelewano na kucheza pamoja.
Lakini watu ambao walitawala nchi wakati huo hawakupenda umoja huu. Watawala hao hawakutaka watu weusi na weupe kuwa marafiki.
Nilijua ilikuwa makosa kuwatendea watu tofauti kwa sababu ya rangi ya ngozi yao.
Sikuficha imani yangu, na kwa hivyo wale watu waliotawala walinitaka niondoke nchini.
Wakati nilikuwa nikiimba huko Amerika, niliambiwa singeweza kurudi nyumbani.
Watu kote ulimwenguni walisikia hadithi yangu. Nyimbo zangu na hadithi yangu ilisaidia wengi kuona jinsi hakukuwa na haki huko Afrika Kusini kwa wale waliokuwa na ngozi nyeusi.
Niliamua kuendelea kuimba na kueleza ukweli kuhusu nchi yangu, bila kujali matokeo yake.
Ulimwengu uliupenda muziki wangu na nilikaribishwa katika nchi nyingi. Nilishinda tuzo na kuwaimbia watu mashuhuri ulimwenguni kote.
Maisha yangu yalikuwa mazuri, lakini kulikuwa na upungufu fulani. Sikuweza kuimba katika nchi yangu, na watu huko hawakuwa huru.
Halafu siku nzuri ilifika wakati Nelson Mandela alikuwa rais wa Afrika Kusini. Watu wapya waliisimamia nchi na sheria zisizo za haki zilizikwa kwenye kaburi la sahau.
Hatimaye, nilikwenda nyumbani nikiwa na matumaini mapya moyoni mwangu.
Baada ya hapo niliweza kuimba katika nchi huru, yenye haki. Watu wenye rangi tofauti za ngozi wangeweza kufurahia muziki pamoja.
Nilisaidia kufanikisha hii kwa sababu nilikuwa shujaa na mwenye nguvu. Niliimba ukweli katika nyimbo zangu zote.


