

Katika mji fulani, kulikuwa na duka nadhifu la viatu vya bei ghali.
Ni katika mji huu ndimo nilizaliwa.
Watu wengi walikuja kwenye duka hilo la viatu, lakini ni wachache tu walioweza kununua viatu hivyo vya mapambo.
Siku moja, mwanamume tajiri mwenye miguu mikubwa alilitembelea duka lile.
Aliziweka pesa zake kwenye kaunta.
Kisha, akiwa ameiweka mikono yake mifukoni, alitembea juu na chini akiviangalia viatu.
Aliponikaribia, nilikosa pumzi na kuganda.
Aliinyosha mikono yake na kunikamata.
Aliketi na kuanza kunivaa kwenye miguu.
Alikuwa na miguu mikubwa, na harufu ilikaribia kunikosesha pumzi!
Nilipakiwa kwenye sanduku.
Tulienda nyumbani, akaniweka kwenye kabati.
Alinivaa kila siku.
Nilimfanya akawa nadhifu na akatembea kwa ujasiri.
Nilikuwa na maisha magumu. Kwa kuwa alikuwa mvivu, hakuiosha miguu yake!
Kwa upande wangu, nilimng'ata wakati mwingine, na kumfanya achechemee.
Mwishowe, nilizeeka na kuvunjika, nikawa na makovu na nyufa.
Aliniweka nje, karibu na pipa la takataka.
Mtu mwingine alinipeleka kwenye karakana ya ngozi ili nichakatwe.
Huko, nilitengenezwa mkoba mpya uliometameta.
Nilianza maisha mapya.

