

Kulikuwa na mvulana mmoja kwa jina Abeli. Alijitengenezea rukwama. Abeli hakuwa na dereva wa rukwama yake mpya.
Akamwambia Meri dada yake, "Nataka dereva wa rukwama yangu. Tafadhali nipe mwanasesere wako. Anaweza kuketi ndani ya rukwama."
Lakini Meri akasema, "Hapana, namtaka mwanasesere wangu." Wakati Meri hakumkubali amchukue mwanasesere, Abeli alikasirika sana.
Alimnyakua mwanasesere na kumvuta. Meri alivuta mkono mwingine wa mwanasesere. Abeli alivuta na Meri akavuta. Mkono wa mwanasesere ukang'oka!
Meri akalia na kukimbia kwa mama yake. "Angalia mama," akasema, "Abeli alivuta mkono wa mwanasesere wangu na ukang'oka. Alitaka mwanasesere wangu aketi ndani ya rukwama yake mpya lakini nilitaka kucheza naye."
Mama yake akasema, "Abeli hakufanya tabia nzuri."
Mama akawaza jinsi ya kumfunza mwanawe kutogusa vitu vya dadake vya kuchezea.
Alikuwa na wazo. Alikwenda kwa rafiki yake ambaye alikuwa daktari na kumwambia, "Tafadhali, nisaidie." Daktari akajibu, "Naweza kukusaidia namna gnai, rafiki yangu?"
Mama akajibu, "Mwanangu Abeli ana tabia mbaya sana siku hizi. Aling'oa mkono wa mwanasesere wa dadake. Hastahili kufanya hivyo.
Kesho nitamwambia akuletee huyo mwanasesere umrudishe mkono tena."
"Tafadhali mwambie Abeli kuwa lazima akulipe kwa kazi yako. Hana pesa zozote, kwa hivyo utamwambia asafishe gari lako kubwa zee ambalo huwa na vumbi kila wakati," mama akasema.
Rafiki yake alicheka na kusema, "Ee-ee! Hilo litakuwa jambo zuri."
Mamake Abeli akarudi kwake nyumbani. Akamwuliza Abeli, ''Unapokuwa mgonjwa au kuwa na maumivu, wewe huenda wapi?" Abeli akajibu, "Wakati mimi ni mgonjwa au nikiwa na maumivu, lazima niende kwa daktari."
Mama akasema, "Ulimwumiza mwanasesere, sasa ni sharti umpeleke kwa daktari."
Kwa hivyo Abeli alimpeleka mwanasesere kwa daktari. "Huyu mwanasesere ameumia vibaya sana. Mama yangu aliniambia nimlete kwako. Daktari, unaweza kumpa mkono mpya?"
Daktari alikubali kumtunza mwanasesere. Aliweza kutengeneza mkono mpya.
Daktari akamwambia Abeli, "Mwanasesere ana mkono mpya. Lazima unilipe. Una pesa ngapi?"
Abeli akajibu, "Tafadhali daktari, sina fedha zozote. Siwezi kukulipa kwa kazi yako."
Daktari akasema, "Vizuri! Huna fedha zozote? Gari langu kubwa ni chafu mno! Lisafishe na hivyo ndivyo utakavyonilipa."
Abeli akachukua ndoo ya maji na kitambaa safi. Ilichukua muda mrefu sana kusafisha gari hilo chafu.
Kisha Abeli akamrudishia Meri mwanasesere wake. Alifurahi sana na kumwambia Abeli, "Wewe ni ndugu mzuri. Asante sana kwa kumtengeneza mwanasesere wangu."
"Dadangu, pole kwa kukasirika na kukuhuzunisha," akasema Abeli.
Tangu siku hiyo, Abeli hakuchukua vitu vya dadake tena. Na akajaribu sana ili asikasirishwe naye.
Abeli alikumbuka muda aliouchukua kusafisha gari lile kubwa, chafu la daktari. Akaamua haikufaa kukasirika na kuvunja vitu.

