

Feni alikuwa msichana mdogo aliyekimbia kama upepo.
Feni alipenda kucheka na alijaribu alivyoweza kutenda alivyoambiwa.
Siku moja, Feni na babake walikwenda shambani kwa baiskeli kung'oa magugu.
Feni alichoka akasema, "Baba, ninahisi joto na uchovu. Niruhusu nipumzike chini ya mwembe."
Baba akajibu, "Ndiyo Feni, unaweza kupumzika pale. Lakini, tafadhali, usipande mti wowote leo."
Feni aliketi chini ya mwembe.
Feni alitazama juu akaona embe moja, maembe mawili, matatu! Yote yalikuwa mabivu.
Feni alimtazama babake. Baba alishughulika na hakuangalia upande wake.
Polepole, Feni alianza kuukwea mwembe. Aliwaza, "Nitapumzikia pahali hapa pazuri nikiyala maembe mabivu."
Kwa hivyo, Feni aliketi akayala maembe.
Baada ya kula maembe, Feni alishuka chini.
Aliuona mti mwingine.
Mti huo ulikuwa ukidondokwa kitu chenye rangi ya hudhurungi.
Kitu hicho kilikuwa asali! Feni alipenda asali mno! Lakini, hakuwependa nyuki.
Feni alitazama juu na kumwona nyuki mmoja mdogo.
Feni aliwaza, "Kuna tu nyuki mmoja mdogo. Hataniumiza nikipanda mtini kutafuta asali."
Feni alimtazama babake. Baba hakuwa akimwangalia.
Kwa hivyo, Feni alipanda juu ya mti na kuchukua asali kutoka shimoni.
Feni aliwaza, "Nitapumzikia pahali hapa pazuri nikiila asali nyingi tamu."
Kwa hivyo, Feni aliketi akaila asali.
Baada ya kula asali, Feni alishuka chini kutoka mtini.
Halafu aliwaona nyuki. Walikuwa nyuki wengi mno! BZZZ! BZZZ! BZZZ!
Feni aliamua kuwatoroka wale nyuki.
Feni alikimbia kumtafuta babake. Alikuwa akihema kweli kweli.
Baba aliuliza, "Feni, umekuwa wapi?"
Feni hakutaka kusema alikokuwa.
Badala ya kumjibu babake, Feni alisema, "Baba, tazama nina embe. Je, ungependa kulila?"
Baba alijibu, "La, asante Feni. Lazima tuondoke kwenda nyumbani sasa hivi. Mvua itanyesha hivi karibuni."
Baba alimbeba Feni kwenye baiskeli wakienda nyumbani. Mvua ilianza kunyesha.
Baba aliendesha baiskeli kwa kasi.
Baiskeli iliiacha barabara.
RURUUU PU!
Baiskeli ilimwangukia Feni mguuni.
Feni aliushika mguu na kulia kwa uchungu!
Walipofika nyumbani, mama na bibi walitaka kujua siku ilivyokwenda walipokuwa shambani.
"Feni alipanda mti," baba alisema.
"Baba aliendesha baiskeli kwa kasi sana hata ikaniangukia mguuni," Feni alisema.
"Aaa, maskini Feni," mama akasema.
"Aaa! Aaa! Maskini Feni! Lazima tuutibu mguu wako," bibi akasema.
Na hivyo ndivyo walivyofanya. Na huo ukawa ndio mwisho wa jambo hilo.

