

Feni alikuwa msichana mdogo aliyekimbia kama upepo.
Feni alipenda kucheka na alijaribu alivyoweza kutenda alivyoambiwa.
Leo ilikuwa Siku ya Michezo shuleni.
Feni alicheza mpira wa miguu na kushindana kwenye mbio aina tatu.
Feni alipotoka shuleni, alitembea na rafiki yake Hawa kurejea nyumbani.
Hawa alimwambia Feni, "Wewe hukimbia kwa kasi!"
Feni aliwasili nyumbani na kumkuta mamake jikoni.
Feni akasema, "Habari ya jioni, Mama."
Mamake akajibu, "Jioni ni nzuri. Habari yako?"
Feni akasema, "Leo ilikuwa Siku ya Michezo shuleni, na nilikimbia kwa kasi. Ninahisi joto, uchovu na nina njaa sana."
Mama akacheka na kusema, "Mpendwa wangu Feni, ulizaliwa na miguu myepesi! Nitatayarisha mchuzi, na chakula cha jioni kitakuwa tayari hivi karibuni."
Mama aliweka mafuta katika chungu kikubwa na kukitia mekoni. Mafuta yalipopata moto, aliongeza vitunguu na saumu, akakoroga hadi vikawa laini.
Aliongeza pilipili, nyanya, maji kidogo na vipande sita vya nyama ya ng'ombe.
Mama akasema, "Feni, tafadhali nisaidie kukoroga mchuzi."
Feni akajibu, "Ndiyo, Mama."
Feni akakoroga mchuzi mara moja.
Akasema, "Mchuzi huu unanukia."
Feni akakoroga mchuzi mara mbili.
Akasema, "Mchuzi huu unanukia sana."
Feni akakoroga mchuzi mara tatu.
Akasema, "Mchuzi huu unanukia sana, sana."
Halafu Feni akamtazama mamake. Mama hakuwa akimwangalia.
Alikuwa akikata mboga za majani kuongeza kwenye mchuzi.
Feni akachukua kipande kimoja cha nyama kutoka chunguni na kukila.
Feni akasema, "Mmm..."
Tena, Feni akamtazama mamake. Mama hakuwa akiangalia upande wake.
Alikuwa akikata mbilingani kuongeza kwenye mchuzi.
Feni akachukua haraka kipande cha pili cha nyama kutoka chunguni na kukila.
Feni akasema, "Mmm... Mmm..."
Kwa mara nyingine, Feni alimtazama mamake. Mama alikuwa ameangalia upande mwingine.
Alikuwa akikata dhania kuongeza kwenye mchuzi.
Kwa haraka, Feni akakichukua kipande cha tatu cha nyama kutoka chunguni na kukila!
Feni akasema, "Mmm... Mmm...Mmm..."
Wakati huo, Mama aliingia jikoni kuongeza mboga ya majani, mbilingani na dhania.
Feni alikuwa bado ameushika mwiko.
Mama akatabasamu na kusema, "Feni, asante kwa kunisaidia kukoroga mchuzi."
Feni hakujua la kusema.
Mama akaongeza mboga ya majani, mbilingani na dhania kwenye mchuzi.
Akauchukua mwiko na kuanza kukoroga mchuzi.
Mama akatazama chunguni. Akavitafuta vile vipande sita vya nyama chunguni.
"Kimoja...viwili...vitatu..." Akaviona vipande vitatu pekee vya nyama. Mama hakusema chochote. Feni hakusema chochote.
Mama alipopakua mchuzi, Feni hakupata nyama yoyote.
Feni akasema, "Nisamehe, Mama. Sitarudia tena." Na kweli, Feni hakurudia tena.
Na huo ukawa ndio mwisho wa jambo hilo.

