Mvumilivu hula mbivu
Abraham Bereket
Adonay Gebru

Katika kijiji kimoja, kulikuwa na mvulana aliyeitwa Abula.

Abula hakupenda kusoma wala hata kufungua kitabu. Licha ya kuwa mwanafunzi mvivu alikuwa na tabia mbovu.

1

Abula alizoea kuiba pesa za mamake na kununua peremende. Hata mama alipozificha, Abula alizipata.

Alipomaliza kula peremende, Abula angeenda kucheza na marafiki zake.

2

Baada ya muda, Abula aliacha kwenda shuleni. Alicheza mchana kutwa na kurudi nyumbani jioni.

Mamake alipogundua jambo hilo, alikuwa na wasiwasi.

3

Alimwambia mumewe, "Mtoto wetu amekuwa mtukutu. Nadhani hata haendi shuleni. Pia ananiibia pesa."

Baba aliwaza jinsi angembadilisha Abula tabia kwa njia mwafaka.

4

Alimwambia mkewe, "Wakati mwingine, zifiche pesa zako katika kurasa za kitabu. Kwa vile yeye hafungui vitabu, pesa zako zitakuwa salama pale."

5

Siku iliyofuata, Abula alitafuta pesa za mamake kila mahali lakini hakupata chochote.

Aliamua kwenda soko iliyokuwa karibu kuona kama angepata pesa zozote.

6

Baba aliona kule Abula alikuwa akienda.

Alisema, "Mwanangu, ninajua kwa nini unakwenda sokoni. Sasa rudi nyumbani ukatafute pesa kwenye vitabu."

7

Abula alishangaa, lakini alikwenda nyumbani akatafuta kwenye vitabu.

Alizipata pesa ambazo mamake alikuwa ameficha.

8

Siku iliyofuata, Abula alitafuta tena kwenye vitabu. Lakini, hakuna pesa zozote zilizokuwa zimefichwa humo.

Alimwuliza babake kwa nini hakupata pesa zozote kwenye vitabu.

9

Babake alitabasamu kisha akamjibu, "Mwanangu, je, ungependa kupata pesa nyingi za kununua vitu vingi vitamu?"

Abula alimjibu, "Bila shaka, baba."

10

Babake alisema, "Nisikilize vizuri. Soma vitabu vyako na uhudhurie shule. Utapata zawadi nyingi kwenye vitabu. Usikate tamaa."

Abula alijibu, "Lakini baba, kusoma ni kazi ngumu. Vitabu vinachosha mno!"

11

Baba aliwaza juu ya kumhamasisha mwanawe. Alimwambia Abula, "Hebu tusome pamoja. Nitakusaidia upate mali vitabuni."

Abula alisoma kwa bidii. Mwishoni, alifaulu na kuishi maisha mazuri.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mvumilivu hula mbivu
Author - Abraham Bereket, Hardido Temesgen, Yohannes Firew
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Adonay Gebru
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs