

Elia aliishi katika nyumba ya kifahari mjini Ebiba. Wazazi wake walikuwa matajiri.
Elia alikuwa na mbwa aliyeitwa Chita. Alimtunza Chita vizuri sana.
Kila siku, baba alimpeleka Elia shuleni na kumrudishi jioni.
Alasiri moja walikuwa njiani kurudi nyumbani. Baba alienda katika duka moja kubwa kununua bidhaa.
Elia alimwona mzee mmoja aliyekuwa amebaba mzigo mkubwa mgongoni.
Alikuwa amechoka kwa hivyo alitembea polepole. Elia aliendelea kumtazama.
Mzee yule aliketi chini ya mti kisha akafungua mzigo ule.
Alichomoa chupa mbili za plastiki akaanza kuzitengeneza viatu.
Elia aliwaza juu ya mzee huyo kwa muda mrefu. Alihuzunika na wala hakuweza kufurahia chakula chake.
Aliwaza, "Nitawezaje kumsaidia?"
Aliamua kuchukua baadhi ya fedha zake. Akamwita Chita halafu akapanda baiskeli yake na kuondoka.
Alienda hadi kwenye lile duka ambako babake alikuwa amenunua bidhaa.
Alinunua vitu vingi akampelekea yule mzee na kusema, "Hujambo babu!"
Mzee alimjibu, "Amani iwe nawe, mwanangu."
Elia akamwuliza, "Babu, unatoka wapi?"
Mzee akamjibu, "Mwanangu, njaa imenifukuza kutoka kijijini kwangu. Nipo hapa kutafuta ajira."
Elia alimpatia bidhaa alivyokuwa amenunua.
Mzee yule hakuamini alipoviona viatu. Alimshukuru Elia kwa moyo wake wote.
Elia alisema, "Sasa lazima nirudi nyumbani kabla mamangu hajaanza kunitafuta."
Elia na mbwa wake walipoondoka, mzee aliwapungia mkono. Alisema kwa tabasamu, "Barikiwa, mwanangu."
Elia alipowasili nyumbani, mamake alimwuliza, "Ulikuwa wapi?" Mama alikuwa na wasiwasi.
Elia alimwambia kila kitu. Mama alimmwonea mwanawe fahari kubwa sana kwa kitendo chake cha ukarimu.
Baadaye, baba alimwambia Elia, "Tunakujivunia, mwanangu. Lakini, ni lazima utuambie kabla ya kuondoka nyumbani. Shika hizi hela utumie kwa sababu ulitumia zako kumsaidia yule mzee!"

