Msichana aliyenuka
Southern African Folktale
Catherine Groenewald

Bahati alikuwa msichana mrembo na nyanyake alimpenda sana.

1

Nyanyake alitumia muda mrefu kumshonea Bahati sketi ya kuvutia.

Bahati alipenda sana kuivaa sketi ile.

2

Wasichana wengine kijijini walimwonea wivu Bahati kwa sababu ya sketi hiyo.

Walipanga kuificha. Lakini, ilikuwa vigumu kuichukua sketi hiyo akiwa ameivaa.

3

Asubuhi moja wasichana hao walimwalika Bahati aende kuogelea nao katika mto uliokuwa karibu.

Walizivua nguo zao na kuziacha ukingoni ili zisitote. Kisha wakajitosa majini na kurushiana maji kwa muda.

4

Baada ya muda, walitosheka kuogelea. Kiongozi wa wasichana wenye wivu, aliirusha sketi ya Bahati majini, karibu na sehemu iliyokuwa na nyoka mkubwa.

Halafu wasichana hao waliondoka na kumuacha Bahati akilia kando ya mto.

5

Mara yule nyoka mkubwa akamsikia akilia. Alijichomoza na kumwona Bahati mrembo.

Nyoka huyo alimmeza Bahati pamoja na ile sketi.

6

Nyoka yule hakuipenda ladha ya sketi, akaitema.  Kwa bahati, akamtema Bahati pia.

Bahati alilala ukingoni mwa mto huku amejifunika kwa sketi yake. Alikuwa amepakwa tope la kunata kutoka tumboni mwa nyoka.

Tope hilo lilinuka fe!

7

Baadaye, Bahati aliivaa sketi yake iliyonuka na kukimbilia nyumbani.

8

Alipofika nyumbani, aliimba:

Mama, nifungulie mlango, miye nanuka;
Mama, nifungulie mlango, miye nanuka;
Miye nanuka fe!

Mama alipousikia wimbo wa Bahati, alimjibu:

Nenda zako Bahati, unanuka;
Nenda zako Bahati, unanuka;
Bahati, unanuka fe!

9

Bahati alihuzunika sana.

Akakimbilia kwa mjombake na shangaziye.

10

Walimsikia akiimba:

Nifungulieni mlango, miye ninanuka;
Nifungulieni mlango, miye ninanuka;
Miye ninanuka fe!

Shangazi na mjomba walimjibu:

Nenda Bahati, unanuka;
Nenda Bahati, unanuka;
Nenda! Nenda! Unanuka fe!

11

Bahati alibaki na wazo moja tu, kukimbilia nyumbani kwa nyanyake.

Lakini, moyo wake ulikuwa mzito. Alijua hakuna aliyemtaka msichana aliyenuka fe.

12

Bahati alikuwa amekosea. Nyanyake hakumfukuza.

Nyanya alimwosha, akaiosha sketi yake, akahakikisha kila kitu kilinukia.

13

Kutoka wakati huo, Bahati aliishi na nyanyake.

Siku moja mvulana tajiri sana alitaka kumwoa Bahati.

14

Wazazi wa Bahati walipofahamishwa kuhusu jambo hilo, walitaka arudi kuishi nao.

15

Bahati alikumbuka jinsi walivyomchukia aliponuka fe.

Aliwaambia, "Sitawahi kurudi nyumbani kwenu tena. Lazima wazazi wawapende watoto wao hata wakinuka."

16

Badala yake Bahati alimwalika nyanyake aende akaishi naye nyumbani mwa mvulana tajiri.

17

Nyanyake alifurahi sana, na wakaishi maisha ya furaha.

18
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Msichana aliyenuka
Author - Southern African Folktale
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Catherine Groenewald
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs