

Sarai ana mtumbwi.
Mtumbwi wake ni mkubwa.
Mtumbwi huo uko kando ya mto.
Baadhi ya wanawake wanafika mtoni. Mwanamke mmoja ana uteo wa matunda. Mwingine ana kuku. Mwingine ana mbuzi mmoja. Wa mwisho ana mbuzi wawili.
Wanamwuliza Sarai, "Tutavukaje mto?"
Sarai anasema, "Ingieni mtumbwi wangu!"
Kisha, wanaume wanafika. Mmoja ana samaki.
Mwingine ana baiskeli.
Mwingine ana gunia la mahindi.
Mwanamume mwingine ana magunia mawili ya mahindi.
Wanamwuliza Sarai, "Tutavukaje mto?"
Sarai anawajibu, "Ingieni mtumbwi wangu!"
Wanyama pia wanakuja. Wanamwuliza Sarai, "Tutavukaje mto?"
Sarai anasema, "Ingieni mtumbwi wangu!"
Wanyama wanaingia mtumbwini. Mbwa anaingia mtumbwini. Paka anaingia mtumbwini.
Tumbili anaingia mtumbwini. Sungura anaingia mtumbwini. Kasa anaingia mtumbwini. Swara anaingia mtumbwini.
Tembo anawasili kando ya mto. Anauliza, "Nitavukaje mto?"
Sarai anasema, "Ingia mtumbwi wangu!"
Tembo anaingia mtumbwini. Mtumbwi unafurika maji.
Salaala!
Mtumbwi umepinduka!
Mtumbwi huu ni mdogo sana.
Hauna nafasi ya kuwatosha wote.
Sarai anasema, "Hebu! Kwanza, nitawavukisha wanawake."
"Kisha niwavukishe wanaume," Sarai anasema tena.
"Hatimaye, nitawavukisha wanyama," Sarai anakamilisha maelezo yake.
Tembo anasema, "Heri nitembee tu!"

