

Kuliishi msichana mdogo katika kijiji kimoja karibu na ziwa.
Aliitwa Atieno.
Babake Atieno alikuwa mvuvi mashuhuri. Alikuwa na mtumbwi wake wa kuvua samaki.
Atieno alifurahi kwenda kuvua samaki na babake.
Atieno aliwatazama wavulana wakicheza mpira wa miguu.
"Hebu nicheze nanyi," aliwashihi siku moja.
Wavulana wale walimcheka, "Nenda ukacheze kidalipo na wasichana wenzako."
Wasichana nao walimwambia Atieno, "Miguu yako ni mirefu mno." Atieno alihuzunika.
Atieno alianza kulichezea jua kila asubuhi.
Jua likawa rafiki yake.
Siku moja, jua halikuchomoza. Jogoo hawakuwika, ndege hawakuimba na watoto hawakwenda shuleni. Hata babake hakwenda kuvua samaki.
Atieno alihuzunika. "Wapi rafiki yangu jua? Kwa nini leo kuna giza?"
Atieno alienda kuwaambia watoto wengine namna alivyohuzunika. Lakini, walimcheka, "Labda jua limefariki. Au pengine limekutoroka."
Atieno aliwajibu, "Jua ni rafiki yangu. Haliwezi kufa."
Atieno alihuzunika sana hata akakimbia kwenda nyumbani. Aliugonga mpira wa kakake kwa makosa nao ulikigonga kibuyu cha mafuta.
Atieno aliwaza, "Nitaucheza mpira huu hadi rafiki yangu jua litakaporudi."
Aliuchukua mpira na kukimbia nao nje.
Atieno alipofika nje, aliuweka mpira chini akawaza, "Ninaweza kucheza kama wao wanavyocheza."
Aliugonga mpira kwa nguvu ukaruka juu angani.
Kila mmoja akitazama juu, mpira ulitokomea kwenye mawingu mazito.
Kulikuwa na kimya kikubwa.
Ghafla, mawingu yaliyokuwa mazito yalipungua na jua likatokezea. Kijiji hicho kikawa hai tena.
Kila mmoja akajitayarisha kufanya kazi aliyozoea kufanya.
Atieno hakuweza kuamini kwamba alikuwa amelirejesha jua kijijini. Lakini zaidi ya yote, jua lilikuwa limerudi maishani mwake.
Aliwaeleza watoto, "Jua ni rafiki yangu na limerudi."

