Mke Mti
Southern African Folktale
Jemma Kahn

Hapo zamani za kale, paliishi mzee aliyekuwa tajiri wa kila kitu. Alikuwa na shamba kubwa lenye rutuba, ng'ombe, na mbuzi.

Lakini jinsi alivyozeeka ndivyo alivyohuzunika kwani hakuwa na mke.

1

Siku moja alipokuwa chini ya mti, alipata wazo zuri sana.

Aliona kuwa ikiwa hatapata mke, labda atajitengenezea mmoja.

2

Alianza kazi ya kumchonga mke kutoka kwa gogo la mti. Alipomaliza kuchonga sanamu, aliyagusa macho nayo yakaanza kuona.

Kisha aliipulizia pumzi sanamu ikawa hai.

3

Akawa mwanamke mrembo zaidi ya wote aliowahi kuona.

Alipiga magoti mbele yake na kumwomba awe mkewe.

4

Yule mume alimvisha kimori, shanga na mkufu wa kichwani, ishara kwamba alikuwa ameolewa. Kisha alimjengea nyumba akitumia matope na nyasi.

"Ninakuomba kitu kimoja tu," mzee yule alisema. "Usimwambie mtu yeyote mahali ulikotoka."

5

Lakini kabla ya kipindi kirefu, vijana kutoka kijiji jirani walianza kusema, "Inawezekanaje mzee kama huyu kumwoa msichana mrembo namna hii!"

Basi wakaamua kumwiba msichana yule na kumpeleka kijijini kwao.

6

Mkewe alipoibiwa, mzee huyo alihuzunika sana. Alihisi kwamba hangeishi bila mkewe. Akawaza, "Labda nikipata kitu chochote kutoka kwake, nitapata faraja."

Aliwatuma njiwa wawili wakamtafute mkewe kisha wamwimbie na wampelekee kitu chochote kutoka kwa mkewe.

7

Njiwa walipomwona, walimwimbia wimbo mtamu:

Mke mti, mke mti,
Mrembo kuliko wote,
Tumetumwa na mumeo,
Tunakujia kimori,
Tukirudishe kwa mumeo,
Asije akakusahau.

8

Aliwapa Kimori chake wakaruka, juu ya milima, juu ya mito, hadi wakarudi kwa mumewe.

Mzee alipokea kimori akakiweka usoni mwake kwa furaha akapata faraja.

9

Faraja hiyo haikudumu. Aliwatuma wale njiwa tena wakamwimbie mkewe:

Mke mti, mke mti,
Mrembo kuliko wote,
Tumetumwa na mumeo,
Tunakujia kimori,
Tukirudishe kwa mumeo,
Asije akakusahau.

Wakarudi wakiwa wamebeba mkufu uliokuwa ishara ya mwanamke aliyeolewa.

10

Aliuchukua ule mkufu akapata faraja ya mke wake aliyekuwa katika kijiji cha watu wengine. Baada ya muda mfupi aliwaita njiwa tena akawatuma kwa mkewe tena wakamwimbie:

Mke mti, mke mti,
Mrembo kuliko wote,
Tumetumwa na mumeo,
Tunakujia kimori,
Turudishe kwa mumeo,
Asije kukusahau.

11

Walienda tena mara ya tatu wakatua mabegani mwake. Walipokuwa wakiimba, kila njiwa alikuwa akidona na kumng'oa jicho.

Punde si punde, akageuka na kuwa sanamu. Miguu na mikono yake ilidondoka. Kichwa vilevile kilianguka.

Akaanguka chini, pu!

12

Mumewe alilisukuma lile gogo la sanamu mtoni. Akalisimamisha upande wa mizizi ukiwa majini.

Na baada ya kupata maji na kupigwa na miale ya jua, lile gogo liliota majani tena kama zamani.

13

Upepo unapovuma, majani yake hushusha pumzi kama vile mwanamke hushusha pumzi anapotamani kumwona mumewe.

14
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mke Mti
Author - Southern African Folktale
Translation - Mutugi Kamundi
Illustration - Jemma Kahn
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs