

Watu kijijini walijua kwamba Mama Schola alipenda kupiga kelele mno.
Siku hiyo, alifanya hivyo kuhusiana na ng'ombe waliokuwa sokoni.
"Wafukuze waende mbali hawa ng'ombe wajinga. Wanakula mboga zangu," alisema.
"Hei we pale! Wafukuze hawa ng'ombe wajinga watoke hapa," alisisitiza. "Wanakula nguo zangu."
"Wapi mwenye ng'ombe hawa wajinga?" alipiga kelele. "Wanakula nafaka yangu."
Kutoka mafichoni, Sorimpan, mchungaji, alichuchumaa kwa kumuogopa Mama Schola.
Alikuwa ameenda kunywa maji wakati ng'ombe wake waliranda na kwenda sokoni.
"Sasa tazama walichofanya hawa ng'mbe wajinga!"
Aliendelea kupiga kelele. "Wamevivunja vyungu vyangu."
Baadaye kidogo, Mama Schola alisema, "Aah! Sio tena! Nitashtaki jambo hili kwa polisi. Hawa ng'ombe wajinga wamekiangusha kibanda changu cha matunda."
Sorimpan, fimbo mkononi, alihepa kati ya umati akfaulu kuwaona ng'ombe wake.
Ng'ombe wa Sorimpan walimjua vyema. Waligeuka na kumwangalia mara tu alipotokea!
Wakati huo, palikuwa na umati mkubwa wa watazamaji: wanaume, wanawake na hata watoto.
Wote walisimama wakiangalia ng'ombe ambao walimtii Sorimapn pekee.
Ghafla, ng'ombe walikivunja kimya chao! Wakaanza kuwakosoa watu!
Watu walishangaa na kupiga hatua nyuma wakiwaogopa ng'ombe.
Kisha ng'ombe waliacha kuzungumza na kuuangalia umati kwa mshangao!
Mama Schola alisikika akisema, "Tangu lini ng'ombe wakaingilia shughuli zetu za sokoni?"
Sasa ilikuwa zamu ya Mama Schola kukosolewa na ng'ombe.
Wanawake wote waliokuwa wakiuza, walisonga na kujiunga na Mama Schola kwa ajili ya woga.
Ng'ombe waliwakosoa wanawake.
Waliongea kuhusu hali ya mboga zao wakisema, "Hizi ni mboga za aina gani? Zitazame jinsi zimeanza kunyauka!"
Ng'ombe waligeuka na kuangalia kibanda cha nguo kisha wakasema, "Mnadai kwamba tunakula nguo zenu! Nguo gani? Hivi viraka vikuu kuu ndivyo nguo! Nani atavinunua?"
Ng'ombe sasa walisongea kibanda kilichofuata. Watu wote waliwafuata.
"Nafaka yenu imejaa wadudu. Nani anataka kuila hiyo! Tulikuwa tuanaonja tu!" Ng'ombe walisema.
Waliendelea, "Nawe Mama Schola, acha kupiga kelele. Vyungu hivi havina thamani yoyote. Vinavunjika upesi. Usitulaumu."
Kisha ng'ombe waliondoka wakifuatwa na Sorimpan.

