Kondoo aliyechoka na maisha ya jijini
Mohammed Alhaji Modu
Kenneth Boyowa Okitikpi

Kondoo aliishi jijini. Alipochoka na maisha ya jiji, aliamua kwenda kichakani.

Njiani, alikutana na Fisi aliyekuwa hajala kwa siku nyingi.

1

Kondoo alisema, "Hujambo ndugu Fisi? Hujambo ndugu Fisi?"

Fisi alimjibu Kondoo, "Usinisalimu ukirudia rudia hivyo. Tenda jambo uitulize njaa niliyonayo."

2

Kondoo aliposikia hivyo, alianza kukimbia.

Alijikuta katika pango la Simba huku akifuatwa na Fisi.

Fisi alifika pangoni huku akimrushia Simba vumbi machoni.

3

Simba alimwambia Fisi, "Kwani hatuwezi hata kupata amani pangoni kwetu? Unaturushia vumbi machoni mwetu!"

Fisi alijibu, "Samahani Mfalme, sikukusudia kukudharau! Ninakifukuza chakula changu!"

4

Simba alisema, "Wewe Fisi, ni chakula kwangu pia. Je, nilikufukuza? Ulikuja wewe mwenyewe. Usinilaumu baadaye."

5

Simba akamwuliza Kondoo, "Mbona ulikuja kichakani?"

Kondoo akajibu, "Nilikuja kwa sababu mimi ni mwaguzi."

6

Simba akasema, "Zitayarishe dawa za kienyeji unihakikishie kwamba wewe ni mwaguzi kweli." Kondoo akajibu, "Dawa zangu ni ghali mno."

Simba akasema, "Hiyo si shida. Hakuna jambo nisiloweza kufanya."

7

Kondoo akasema, "Sikio la Fisi ndilo dawa."

Simba akalikata sikio la Fisi na kumpatia Kondoo.

Kondoo akaliweka sikio hilo ndani ya chupa iliyokuwa na asali. Kisha akampatia Simba.

8

Simba alipolila lile sikio, lilikuwa tamu sana.

Akamwuliza Kondoo, "Inawezekana kulipata sikio la pili?"

9

Kondoo akasema, "Ndiyo, inawezekana mfalme wangu." Kwa hivyo, Simba alilikata sikio la Fisi la pili akampatia Kondoo.

Kondoo akaliweka tena ndani ya chupa iliyokuwa na asali kisha akampatia Simba.

10

Simba akamwuliza Kondoo, "Je, inawezekana kuipata ngozi?" Kondoo akajibu, "Nadhani inawezekana mfalme wangu."

Fisi aliposikia hivyo, aliogopa kufa. Alitoroka huku akifukuzwa na Simba.

11

"Ikiwa hivyo ndivyo maisha yalivyo kichakani, heri nirudi nyumbani," Kondoo alisema.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Kondoo aliyechoka na maisha ya jijini
Author - Mohammed Alhaji Modu
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Kenneth Boyowa Okitikpi
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs