

Kuliishi mfalme katika Kisiwa cha Rusinga. Mfalme huyo hakuwa amehisi maumivu maishani mwake.
Hakuwahi hata dakika moja.
Asubuhi moja mfalme alikiinamisha kichwa chake. Aliwaza namna maumivu yanavyokuwa. "Kuna watu wengi maskini katika ufalme wangu. Nitawezaje kuhisi maumivu yao?" alijiuliza.
Mchana na usiku, alitamani kuhisi maumivu angalu mara moja tu.
Usiku mmoja, aliota ndoto akasikia sauti ikisema, "Nimesikia matakwa yako. Utahisi maumivu."
Sauti hiyo iliendelea, "Yajenge mashua kubwa saba ambamo utaweka mali na familia yako. Kisha safiri ukielekea upande wa kaskazini mwa Kisiwa cha Rusinga."
Mfalme alifurahi sana.
Muda mfupi baadaye, mashua saba yalijengwa na wakawa tayari kusafiri.
Siku moja kabla ya safari, mfalme aliandaa sherehe. Kila mmoja alihudhuria. Chui, nyoka, sungura, konokono, ndege na hata siafu, wote walifika kwa sherehe.
Mfalme aliwahotubia watu, "Mimi na familia yangu tunaondoka kwenda sehemu tofauti ya Kisiwa cha Rusinga. Tunataka kuhisi maumivu ambayo watu wengine huhisi."
Watu walinong'onezana miongoni mwao. Wazee hawakumwamini.
Lakini, ni nani angemhoji mfalme?
Siku iliyofuata, mfalme na familia yake walisafiri.
Kwa siku mbili, mashua yalipita majini. Anga lilikuwa wazi, bahari ilitulia na safari ilifurahisha.
Lakini siku ya tatu, bahari ilichafuka. Anga lilibadilika likatanda mawingu. Walikumbwa na dhoruba kubwa.
Mashua yalizama. Mfalme hakuweza kufanya lolote. Familia na mali yake ilipotelea baharini.
Mfalme pekee alinusurika. Lakini, alikuwa amebadilika na kuwa mdiria.
Mdiria aliruka akatua ukingoni mwa bahari. Alikuwa bado akitumaini kuipata familia na mali yake kutoka baharini.
Mdiria alipiga mbizi baharini mara nyingi. Hakuweza kuiokoa familia yake au hata baadhi ya mali yake.
"Kama ningejua, ningeyafurahia maisha yangu yalivyokuwa," alilia.

