Watu waliosahau
Edwin Irabor
Edwin Irabor

Hapo zamani za kale, kulikuwa na kijiji kilichoitwa Raha. Watu wote walikuwa vijana.

Hapakuwa na mwanamume wala mwanamke mkongwe kijijini humo.

1

Vijana wa kike na wa kiume kijijini Raha walicheza na kufurahi. Walikula walichopenda na kunywa chochote kilichowalevya. Walifurahi mchana kutwa na usiku kucha.

Hivi karibuni, walisahau namna ya kufanya kazi.

2

Pia walisahau chochote kilichotendeka siku iliyopita.

Siku moja vijina wa kijijini Raha waliamka na kukuta kuwa chakula chote kilikuwa kimeisha. Hapakuwa hata na tone moja la mvinyo. Ala zote za muziki zilikuwa zimevunjika.

3

Hapakuwa na muziki wa kucheza. Hata hawangeweza kucheza kwa sababu walihisi njaa na kudhoofika.

Walienda kwa Oza, chifu wa kijiji, na kulia kwa uchungu.

4

Chifu wao kijana alitoka nje ya chumba na kuwasihi, "Acheni! Watu wapendwa wa kijiji cha Raha. Tafadhali acheni kulia. Tutaweza kufa hivi karibuni. Heri tutumie nguvu tulizo nazo kubaki hai."

5

Watu walipiga kelele, "Wewe ni chifu wetu! Lazima utuokoe!"

Baada ya kunyamaza kwa muda, chifu Oza alisimama akasema, "Mimi si chifu wenu tena. Nitaondoka hapa nitafute pahali palipo na amani. Mnaweza kumchagua chifu mwingine."

6

Kwa hivyo, chifu Oza aliingia chumbani kwake akakusanya virago vyake na kuondoka.

Watu hawakujua nani angekuwa kiongozi wao. Hawakujua la kufanya. Walilia zaidi.

7

Halafu sauti ndogo na nyororo ikasema, "Nitakuwa chifu wenu!"

Kila mmoja aligeuka kujua aliyeitoa sauti ile. Wote waliangaliana. Walitazama kila mahali lakini hawakumtambua aliyekuwa amezungumza.

8

Watu hao walishangaa kumwona mtoto mdogo mbele yao.

Mtoto huyo alisema, "Ndiyo! Nitakuwa chifu wenu. Ninaweza kuwasaidia. Lakini, lazima mniahidi kuwa mtakoma kusherehekea mchana na usiku. Tena, lazima mfuate ushauri wangu."

9

Watu hao walivutiwa sana na ujasiri wa mtoto huyo. Wakaahidi kumtii.

Akawapeleka katika shamba lililokuwa na rutuba. Wakala, wakanywa na wakapumzika. Halafu, akawafunza na kuwakumbusha jinsi ya kulima.

10

Wakisaidiwa na yule mvulana mdogo kama chifu wao, watu wa kijijini Raha, walianza kujifunza maana ya jitihada. Walifanya kazi kwa bidii.

Baadaye, walipata chakula na vinywaji vya kutosha. Walifurahi na kusherehekea tena. Lakini, pia, waliendelea kufanya kazi.

11

Kila usiku, yule chifu mdogo aliondoka kijijini na kukutana na mzee mwenye busara.

Alimhadithia kuhusu wanaume na wanawake shujaa waliotatua matatizo ya watu wao.

Hatimaye, mvulana huyo, alikuwa mtu mwenye hekima na mwenye uwezo mwingi.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Watu waliosahau
Author - Edwin Irabor
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Edwin Irabor
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs