

Hapo zamani, kulikuwa na mvulana aliyeitwa Jalo. Jalo aliwaasi wazazi wake.
Watu walijua kuwa mvulana huyo alikosa adabu.
Siku moja Jalo na mamake waliwatembelea jamaa zao kijijini.
Kabla wao kuondoka kurejea nyumbani, jamaa zao waliwapatia zawadi.
Walimpeleka Jalo na mamake kwenye bustani iliyojaa matunda. Kisha wakawaalika kula matunda yoyote waliyopenda.
Ila, hawakutakiwa kuchuma kutoka kwa mwembe.
Jalo aliona mwembe mkubwa uliokuwa na maembe mengi mabivu.
Jalo alishangaa kuyaona maembe mengi mabivu. Aliamua kuchuma moja.
Ingawa Jalo alikuwa ameonywa kutokula kutoka kwenye mwembe, alifanya hivyo.
Alisema, "Litakalofanyika, lifanyike. Ninataka kulila embe hili."
Mamake Jalo alimwonya tena. Hata hivyo, Jalo hakumtii.
Alipolila tu hilo embe, tumbo ilianza kunguruma.
Jalo aliendelea kuhisi vibaya akaanza kulia. Kichwa chake kilianza kuvimba.
Halafu, mwembe uliota kichwani kwake! Jalo aligeuka na kuwa mwembe.
Tangu wakati huo, kila mwembe huo unapoguswa, huimba, "Asiyewatii wazee, atajuta. Jalo ni mfano."
Hivyo ndivyo ilivyo. Wahenga husema, "Asiyesikia la mkuu, huvunjika guu."

