Siku ya Betina
Ursula Nafula
Catherine Groenewald

Betina alikuwa amelalia mkeka wake. Alimsikiliza mamake akimsimulia hadithi aliyoipenda zaidi.

Hadithi iliwahusu wanawake waliojulikana mle kijijini kwa mikeka na vikapu maridadi waliyotengeneza.

Betina aliithamini zawadi ya mkeka aliyopewa na bibi alipohitimu umri wa miaka kumi.

1

Betina aliposimama, mamake alitaka kuuweka makeka wake. Betina alisema, "Mama, usiukunje sasa. Hebu kwanza tutazame rangi na maumbo yaliyoko."

Betina alizitaja rangi kwenye safu zote kutoka juu hadi chini, "Waridi, waridi, kijani, kijani, bluu, bluu, waridi, waridi, kijani, kijani." Ni sehemu gani ya mkeka ambapo muundo unabadilika?

2

Betina aliukunjua mkeka. Maumbo mengi yalikuwa mistatili na mengine miraba. Alisema, "Ninajua njia rahisi ya kupata jumla ya maumbo yote. Si lazima kuhesabu kila umbo, bali unahesabu idadi ya maumbo yaliyo kwenye kila mstari."

Je, unajua namna Betina anayahesabu maumbo hayo? Kuna jumla ya maumbo mangapi?

3

Betina alikuwa na mkeka mwingine mdogo alioutumia kuketi nje. Huo ulikuwa na mistatili pekee. Betina anaweza kuwa ameifunika kwa mwili wake takriban mistatili mingapi? Takriban mistatili mingapi ambayo haijfafunikwa?

Unaweza kutumia njia ya Betina ya haraka kupata mistatili mingapi ambayo mkeka huo unayo?

4

Asubuhi moja, Betina alienda kumtembelea bibi. Aliwakuta wanawake kisimani wakiwa wamebeba maji vichwani.

Alishangaa akataka kujua ni maji lita ngapi yaliyokuwa katika kila ndoo. Je, unafikiriaje?

5

Betina alipowasili, bibi alimkaribisha, "Betina, furaha ilioje! Hiki ni kikapu kipya nilichotengeneza. Unakipenda?" Betina alimjibu, "Ninapenda rangi yake, lakini sipendi maumbo yaliyoko."

Utawezaje kuchora maumbo yaliyoko kwenye kikapu hicho? Maumbo hayo yanafanana mraba au mstatili au umbo jingine tofauti?

6

Alipokuwa akirudi nyumbani, Betina aliikosa njia. Hakujua alikokuwa kwa hivyo, aliketi chini ya mti kupumzika.

Aliyatazama majani yakicheza juu yake kwenye matawi. Aliyaona maumbo tofauti yaliyosababishwa na mwangaza yakicheza kila mahali. Baadaye, alipatwa na usingizi mnono.

7

Betina alipoamka, aliogopa. Alitaka kuwa nyumbani na mamake akipumzika kwenye makeka wake.

Wakati huo huo, ndege mdogo wa rangi ya bluu alitua mtini. "Hujambo. Usiwe na wasiwasi, nitakusaidia ufike nyumbani. Nifuate," yule ndege alisema.

Betina alishangaa kumsikia ndege akiongea.

8

Betina alimfuata yule ndege hadi kwenye njia panda. Njia iligawika, moja ikienda kushoto na nyingine kulia. Je, aifuate njia gani?

Betina alitazama juu. Iliwezekana kuwa yule ndege alikuwa amebeba mdomoni kipande cha mkeka wake! Ndege yule alikiangusha kile kipande kwenye njia iliyokwenda upande wa kulia, kisha akaenda zake.

9

Betina aliifuata njia hiyo akapanda mlima na kushuka. Aliwasikia watu wakicheka na kuimba kijijini kwao.

Betina alifurahi alipofika nyumbani salama.

10

Mamake aliukunjua mkeka kisha akampa chakula. Betina aliyahesabu maumbo ya miraba yaliyokuwa kwenye mkeka kuhakikisha kwamba yalikuwa bado yako.

Alikuwa na uhakika kwamba alikiona kipande cha mkeka kilichokuwa kimekatwa. Alijua hakuwa akiota. Ilikuwa kweli kuwa yule ndege mdogo alikuwa amemwokoa!

11
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Siku ya Betina
Author - Ursula Nafula
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Catherine Groenewald
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs