Maswali aliyouliza Katiti
Jean de Dieu Bavugempore
Rob Owen

Katiti alipenda kuuliza maswali. Aliyapata mazoea haya kutoka kwa wazazi wake.

Waliokuwa wakimwambia, "Usipouliza maswali ukiwa mdogo, utakapokua mtu mzima, utakuwa mjinga!"

1

Siku moja, Katiti alimwuliza mwalimu wake, "Kwa nini wazazi wetu wanatueleza kila wakati tuwe tukinawa mikono yetu kabla ya kula, hata kama mikono yetu huonekana kuwa misafi?"

Wenzake darasani walilipenda swali lake. Wao pia hawakupenda kuambiwa kunawa mikono yao.

2

Mwalimu alijibu, "Hilo ni swali nzuri, Katiti. Mikono yetu hata inapoonekana kuwa misafi, inaweza kuwa na viini."

Mwalimu aliwaeleza wote, "Viini husababisha maradhi. Hatuwezi kuviona viini hivyo kwa macho yetu. Tunahitaji kifaa kilicho na nguvu zaidi ili tuvione."

3

Mwalimu aliichukua darubini kutoka kabatini. "Darubini ni kifaa tunachotumia kuviona vitu vilivyo vidogo sana ambavyo hatuwezi kuviona kwa macho yetu," alisema.

Kwa utaratibu, mwalimu aliifuta mikono ya Kariza kwa kijiti. Halafu, akakifutia kile kijiti kwenye kioo cha darubini.

4

Mwalimu alikiweka kile kioo juu ya darubini.

Hiki ndicho walichoona walipotazama. Hata kama mikono ya Katiti haikuonekana kuwa michafu, ilikuwa na viini chungu nzima juu yake.

5

"Kuna viini kila mahali. Vinapatikana kwenye vitu tunavyogusa, darasani kwetu, uwanjani na hata nyumbani. Viini hivi vinaweza kutufanya tuwe wagonjwa," mwalimu aliwaonya.

6

Mwalimu aliendelea, "Ili kuviangamiza viini hivi, lazima tuioshe mikono yetu kwa maji safi na sabuni, hasa kabla ya kula. Pia, tunapokuwa wagonjwa, lazima tuioshe ili tusivieneze viini."

7

Katiti alipofika nyumbani, alimkuta babake akiwa anatengeneza kiti cha aina ya pekee.

Akamwuliza, "Baba, unatengeneza nini?" Babake alimjibu, "Hiki kinaitwa 'chukua hatua unawe'. Unakitumia kunawa mikono yako baada ya kukitumia choo na kabla ya kula."

8

Katiti alishangaa akasema, "Ndiyo! Mwalimu wetu ametuambia kuhusu kifaa hiki, lakini wengi wetu hatujui jinsi ya kukitumia. Kinatumikaje?"

Babake alicheka halafu akamwambia, "Hebu njoo binti yangu nikuonyesha."

9

"Kwanza kabisa, kikanyage kipande hiki cha mti kilichoko sakafuni," baba akasema.

10

"Unapofanya hivyo, mtungi wa maji utainama na kuyamwaga maji mikononi kwako. Kumbuka kuitumia sabuni kunawa," baba akamwambia Katiti.

11

Katiti alifurahi akasema, "Ningejuaje jambo hili nisingeuliza maswali? Ni kweli kwamba maswali humwelekeza mtu kupata maarifa."

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Maswali aliyouliza Katiti
Author - Jean de Dieu Bavugempore
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Rob Owen
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs