

Katika mwaka mmoja, kipindi cha ukame kilikuwa kirefu sana. Kiangazi kikawaathiri wanyama wote. Mito yote ikakauka ila Mto wenye Baraka.
Wanyama wakahisi kiu kikubwa wakaamua kukutana ili watafute suluhu.
Ngamia alikuwa wa kwanza kuzungumza, "Kama mnavyojua, tuna kiu kikubwa na mito yote imekauka ila Mto wenye Baraka. Lakini mto huo uko mbali sana. Je, tufanyaje?"
Farasi alitoa pendekezo, "Baadhi yetu tunaweza kwenda kwenye Mto huo wenye Baraka. Tutaweza kuyanywa maji na kisha tuwaletee wengine."
Ng'ombe alijibu, "Ni mbali sana. Tutakaporudi, wale tutakaokuwa tumewaacha nyuma, watakuwa wamefariki."
Mbuzi aliruka juu kisha akasema, "Meee, meee! Mimi pia nitaenda kwenye Mto wenye Baraka."
Jimbi naye akasema, "Koor, kor kor kor! Pia mimi nitaenda kwenye Mto wenye Baraka."
Haikuwa rahisi kwenda huko. Aliyekuwa nyuma ya wote, alikuwa Kanga. Baada ya kutembea kwa muda mrefu, Kanga alisema, "Rafiki zanguni, siwezi tena kuendelea kwenda kwenye Mto wenye Baraka."
Jimbi akammeza Kanga.
Waliendelea na safari tena. Muda mfupi baadaye, Jimbi akasema, "Tafadhali, nimechoka. Siwezi tena kuendelea kwenda kwenye Mto wenye Baraka."
Kondoo akammeza Jimbi.
Safari ilipoendelea, Kondoo alichoka kisha akasema, "Nimechoka. Sitaki tena kuendelea kwenda kwenye Mto wenye Baraka."
Mbuzi akammeza Kondoo.
Punde tu, Mbuzi naye alichoka na hakutaka kuendelea kuendelea kwenda kwenye Mto wenye Baraka. Farasi aligeuka na kummeza Mbuzi.
Farasi alipochoka, Ng'ombe alimmeza.
Sasa walikuwa wamebaki Ng'ombe na Ngamia peke yao. Waliendelea na safari hadi Ng'ombe alipochoka.
Ilimbidi Ngamia ageuke na kummeza Ng'ombe.
Ngamia alipobaki peke yake, alijitahidi ili aufikie Mto wenye Baraka. Ni yeye tu ndiye angeweza kuwaokoa wengine.
Alikuwa amechoka mno.
Hatimaye, Ngamia aliwasili kwenye Mto wenye Baraka na kulala chini. Kisha akamtapika Ng'ombe.
Ng'ombe akamtapika Farasi. Farasi akamtapika Mbuzi.
Mbuzi akamtapika Kondoo. Kondoo akamtapika Jimbi naye Jimbi akamtapika Kanga.
Na hivyo ndivyo wanyama wote walivyofaulu kuyanywa maji kutoka Mto wenye Baraka.

