Aku, rafiki ya Jua
Aisha Nelson
Idowu Abayomi Oluwasegun

Hapo zamani, kuliishi msichana mmoja katika kijiji kilichoitwa Nchijua.

Msichana huyo aliitwa Aku. Alikuwa msichana mwenye miguu mirefu mno.

Aku alistaajabishwa na mambo mengi.

1

Babake Aku aliitwa Juma na alikuwa mvuvi. Wakati mwingine, Juma alienda na Aku kuvua samaki.

Alipofanya hivyo, Aku alistaajabu kwa nini kila mara jua lilimtazama kutoka juu angani.

Mara nyingine Aku alimsaidia mamake, Agatha, kupika. Alipofanya hivyo, alistaajabu kwa nini mafuta yalikuwa rangi nyekundu yalipokuwa kwenye kibuyu lakini kuwa manjano yakiwa kwenye viazi vikuu.

2

Pia, Aku alistaajabu kwa nini Oti, kakake, na wavulana wengine hawakumruhusu acheze nao mpira wa miguu.

Aku alipowauliza kwa nini, walicheka kisha wakamwambia aende acheze na wasichana wenzake.

Wasichana nao hawakutaka kucheza naye. "Miguu yako ni mirefu sana," walimwambia Aku kila mara.

3

Aku alifanya urafiki na Jua. Alitazamia kuliona Jua kila alipoamka asubuhi. Jogoo walipowika kutangaza mawio, Aku alichezea juani huku kivuli chake kikicheza naye.

Kuimba kwa ndege na kuwika kwa jogoo ilikuwa muziki mtamu kwake. Jua lilimfurahisha na kumfanya atabasamu.

Lakini siku moja, Jua halikuchomoza.

4

Aku alisubiri jogoo kuwika, lakini, hawakufanya hivyo. Ndege hawakuimba. Bila Jua, watu wa Nchijua hawakutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Wakulima hawakukuza mimea yao. Anga liligeuka kijivu likahuzunika. Juma hakwenda kuvua samaki. Watoto hawakwenda shuleni. Wanawake hawakujadiliana bei za bidhaa sokoni.

Aku alivikosa vitu hivyo vyote. Alikosa kuwika kwa jogoo na nyimbo walizoimba ndege. Alichokikosa zaidi, ni kuchomoza kwa Jua.

5

Kila mmoja alitaka kujua Jua lilienda wapi. "Labda Jua limefariki," baadhi yao walisema. "Jua limesafiri," wengine wakasema. Wengine walimcheka Aku.

Hata hivyo, Aku alijipa moyo, "Ninasema ukweli. Jua ni rafiki yangu. Jua halijafariki."

Lakini, hakuna yeyote aliyemsikiliza zaidi. Walisahau Jua wakamcheka Aku kwa nguvu. Kilichomhuzunisha zaidi ni kule kuchekwa na watoto wenzake.

6

Akiwa amehuzunika kama vile Jua lilivyokuwa, Aku alifanya hima akaenda nyumbani. Aliugonga mpira wa kakake kimakosa. Mpira uliviringika na kuingia jikoni.

Mpira ulikigonga kibuyu cha mafuta kilichokuwa jikoni kikaanguka chini. Mafuta yalimwagika nao mpira ukaloa.

7

Oti na rafikiye mmoja waliingia jikoni kuuchukua mpira wao. Walikiona kibuyu kilichokuwa kimeanguka na mafuta yaliyomwagika. Mpira wao ulikuwa umeloa.

Oti, Agatha na watu wote wa Nchijua walimtazama Aku akitoroka. Walistaajabu wasijue alichopanga kuufanyia mpira ulioloa mafuta.

8

Aku alisimama alipofika katikati ya uwanja. Akauweka mpira chini na kwa nguvu zote, akaugonga kwa mmoja wa miguu yake mirefu.

Mpira ukazunguka chini ukaelekea mwishwo wa uwanja. Ukaugonga mizizi ya mtende mmoja uliokuwa mwisho wa uwanja.

9

Mpira huo ulielekea angani. Wakiwa vinywa wazi, watu wa Nchijua waliutazama mpira ukiruka mbali na mawingu, mbali na upeo wa macho yao. Kila kitu kikatulia. Kukawa na kimya kikubwa.

Ghafla, anga lilifunguka. Mawingu yakawa kama pamba nyororo. Mpira mkubwa ukapenyezea nyuma ya mawingu.

Mpira huo uliokuwa mwekundu na manjano kama mafuta, ukang'aa. Mpira huo ulikuwa Jua, rafikiye Aku. Kila kitu kilisisimuka. Kimya kikamalizika.

10

Kila mtu alifanya hima kwenda nyumbani kujitayarisha kwa shughuli za kawaida.

Juma alitafuta ndoo yake ya samaki. Wakulima waliyachukua majembe yao. Watoto walioga na kuvaa tayari kwenda shuleni.

Wanawake walijifunga kanga zao. Walibeba vikapu wakaenda haraka sokoni.

11

Jua lilirejea Nchijua.

Aku alikuwa amefaulu.

Siku mpya ilianza…

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Aku, rafiki ya Jua
Author - Aisha Nelson
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Idowu Abayomi Oluwasegun
Language - Kiswahili
Level - Read aloud