

Siku moja, mvua kubwa ilikuwa imenyesha. Imani alitazama angani na kwa mara ya kwanza, aliona rangi.
Rangi zile zilipendeza sana. Alidhani kuwa mtu fulani alikuwa amefanya kazi kubwa ya kuipaka anga rangi kama vile babake alivyozipaka nyumba.
Alikimbia kumweleza dadake. "Sarah, tazama! Mtu fulani ametupakia anga rangi na kuirembesha."
Lakini Sarah alisema, "Usiwe mshenzi! Huo ni upinde. Wewe ni mdogo nami ni mkubwa. Ninajua kwa nini upinde uko angani. Hebu nikuonyeshe."
Alimpeleka Imani katika bustani ya wanyama akasema, "Upinde hautokezei kwa sababu simba wananguruma kwa mara ya kwanza. Wala hautokezei kwa sababu tembo wanazaliwa."
Sarah alimpeleka tena Imani kwenye bustani ya maua akasema, "Upinde hautokezei eti kwa sababu vipepeo wameipoteza rangi yao mawinguni."
Sarah alimwonyesha Imani kitabu akasema, "Vilevile, upinde hautokezei eti kwa sababu vifaru wanakimbia na kuzitisha rangi."
"Ninajua kwa nini pinde hutokezea. Mama alinieleza, nami sasa ninakueleza!" Sarah alimwelekeza Imani kwenye uwanja wa michezo.
"Pinde hutokezea angani kwa ajili ya watoto kama mimi na wewe. Siku moja, rangi zilitazama chini kutoka juu na zikafurahia kile zilizoweza kuona."
"Ziliwaona watoto wenye rangi ya maji ya kunde, rangi nyeusi na rangi iliyo katikati. Ziliwaza, 'Ni ajabu ilioje kupendeza kama watoto hawa wanavyopendeza.'"
"Rangi hizo zilikuja pamoja angani zikajadiliana ambavyo zingefanya. Ziliamua, 'Tutaweza tu kupendeza tukiwa kikundi.'"
"Sasa, huwa zinaungana pamoja na kung'ara namna zinavyoweza. Zina matumaini ya kupendeza kama watoto zinazoona, watoto kama mimi na wewe."

