Jinsi kahawa ilivyogunduliwa
Alemu Abebe
Mekasha Haile

Mkahawa huzaa matunda yaliyo na mbegu ndani. Mbegu hizo ni kahawa.

Kuna hekaya nyingi kuhusu jinsi kahawa ilivyogunduliwa. Mojawapo inamhusu Kaldi, raia wa Ethiopia.

1

Kaldi alikuwa mchungaji nchini Ethiopia. Inasemekana kuwa siku moja mbuzi wake waliyala matunda ya rangi nyekundu kutoka mti wa kahawa.

Baadaye, Kaldi alishuhudia mbuzi hao wakirukaruka kwa uchangamfu usiokuwa wa kawaida.

2

Kaldi alikuwa na hamu kubwa ya kutaka kujua ikiwa matunda yale yaliwapa mbuzi wake nguvu fulani.

Alionja ladha yake chungu alipoyatavuna.

3

Baadaye, Kaldi alikuwa macho. Yeye pia alihisi nguvu fulani mpya.

4

Alichuma baadhi ya majani na yale matunda.

Aliyapeleka nyumbani na kumpatia mkewe.

5

Mkewe alipoyatavuna yale matunda, naye pia aliathirika kama Kaldi. Alikuwa macho na kuhisi nguvu ya kipekee.

Kaldi na mkewe waliamini kuwa matunda yale yalikuwa zawadi kutoka kwa Mungu.

6

Siku chache baadaye, Kaldi aliwapelekea watawa matunda yale na majani yake.

Aliwahadithia jinsi mbuzi wake walivyoathirika walipoyala matunda yale.

7

Alipoondoka, watawa wawili walimfuata kisirisiri wakitaka kujua ikiwa ilikuwa ukweli.

Walihakikisha walipowaona mbuzi wakichangamka na kucheza baada ya kuyala yale matunda.

8

Watawa walirudi nyumbani na kuyachemsha yale matunda ya kahawa.

Walipoyanywa maji yaliyochemka, ladha yake ilikuwa chungu sana! Walidhani kuwa kilikuwa kinywaji cha shetani.

9

Waliyatupa matunda yaliyobaki kwenye moto. Yalipochomeka, walinusu harufu yake nzuri.

Walipata wazo la kuzikaanga zile mbegu kwanza kabla ya kuzichemsha.

10

Kinywaji kilichotoka kwenye mbegu zilizokaangwa kilikuwa na ladha nzuri zaidi.

Baada ya watawa kunywa kinywaji kile, walikuwa macho na wenye nguvu.

11

Tangu wakati huo, watu hunywa kahawa ili kuwa macho na pia kuburudika.

Kwa hivyo, unywaji wa kahawa ulianzia nchini Ethiopia na kuenea ulimwengu mzima!

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Jinsi kahawa ilivyogunduliwa
Author - Alemu Abebe, CODE Ethiopia
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Mekasha Haile
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs