Masanduku matatu yenye mali
ሰለሙን
Adonay Gebru

Kulikuwa na mzee mmoja aliyeitwa Hagos. Aliishi na wanawe watatu.

Hagos alitaka wanawe wawe na mali baada ya kifo chake. Alitayarisha masanduku matatu.

1

Hagos alikwenda kwa Haile, jirani yake, na kumwambia, "Ninataka wanangu wawe na mali.
Nimeyatayarisha masanduku matatu. Ningependa uwapatie masanduku hayo baada ya kifo changu."

2

Baada ya Hagos kufariki, Haile aliwaita pamoja wale ndugu watatu akawaeleza, "Kabla baba yenu kufariki, alinipatia haya masanduku matatu. Kila sanduku lina jina. Naomba kila mmoja alichukue sanduku lililo na jina lake."

3

Ndugu wale walichukua kila mmoja sanduku lake kisha wakayafungua.

Sanduku la kwanza lilikuwa na dhahabu. La pili, lilikuwa na udongo. Nalo la tatu lilikuwa na samadi.

4

Aliyepata dhahabu alifurahi sana. Waliopata udongo na samadi, hawakufurahi. Walianza kugombana na yule aliyepata dhahabu.

5

Haile aliwaambia, "Ninyi ni ndugu na hamstahili kugombana. Hebu niwapeleke kwa mzee mwenye busara awashauri."

6

Haile aliwapeleka ndugu wale watatu kwa mzee mwenye busara. "Habari za asubuhi. Tumekuja kwako kutafuta ushauri kuhusu urithi," Haile alimweleza yule mzee.

7

Haile alimwambia yule mzee mwenye busara kuhusu yale masanduku matatu ambayo Hagos aliwaachia wanawe.

"Sasa hawa wawili, wanagombana na yule aliyepata sanduku lililokuwa na dhahabu," Haile alieleza.

8

Yule mzee mwenye busara alisizitiza, "Baba yenu alikuwa na sababu ya kuwapatia sanduku ambalo kila mmoja wenu alipata."

9

Aliendelea kuwaeleza, "Wewe ulipata dhahabu kwa sababu babako alitaka uwe mfanya biashara. Nawe ulipata udongo kwa sababu babako alitaka uwe mkulima."

10

"Wewe ulipata samadi kwa sababu babako alitaka uwe mchungaji. Baba yenu alitaka mfanye kazi yenu kulingana na vipaji vyenu," mzee mwenye busara alikamilisha maelezo yake.

11

Baada ya kusikiliza ushauri wa yule mzee mwenye busara, wale ndugu watatu walikubaliana naye. Kila mmoja wao aliifanya kazi yake tofauti na wakaishi kwa furaha.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Masanduku matatu yenye mali
Author - ሰለሙን, ተኹሉ ይግዛው
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Adonay Gebru
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs