Zawadi ya Sisanda
Gcina Mhlophe

Sisanda ni msichana wa umri wa miaka minane. Kila siku anapotoka shule, anavua sare, anakula chakula cha mchana kisha yeye na babu yake wanacheza mchezo waupendao.

Wanafurahia sana kucheza hadi Sisanda hataki kuacha.

Babu anamkumbusha kuwa angependa kuwa meneja wa benki atakapokuwa mkubwa.

1

Babu anamwuliza kwa utani, "Utawezaje kuwa meneja wa benki usipokwenda shule ya upili?"

Sisanda anacheka tu. "Nitamaliza masomo ya shule ya upili na hata niende chuo kikuu. Hiyo ndiyo sababu ninatia bidii sana masomoni!"

2

Sisanda ni mrefu kwa umri wake. Anafuata urefu wa babake. Anamfanana mamake kwa uso wake ulio mfiringo na kwa tabasamu yake.

Kila siku wazazi wake huamka mapema na kwenda kwenye hifadhi ya wanyama iliyo karibu wanakofanya kaz.

Wakati Sisanda na rafiki zake wanapoanza kwenda shule, mabasi huwa tayari yamewafikisha watalii kwenye hifadhi hiyo ya wanyama.

3

Maadhimisho ya kuzaliwa kwake iliyopita, Sisanda aliandaliwa sherehe maalum. Wazazi walipata ruhusa ya kuandaa sherehe hiyo katika hifadhi ya wanyama.

Twiga walivutiwa sana na watu waliofika kwenye sherehe hiyo. Waliyanyoosha mashingo yao marefu wakaiona sherehe vizuri na kutaka kuptata sehemu ya keki!

Sisanda aliwapenda twiga zaidi ya wanyama wote kwa ajili ya upole na utulivu wao. Angewatazama kwa siku nzima.

4

Ijumaa moja, babake Sisanda alikuja nyumbani mapema kutoka kazini. Alionekana kuwa mwenye hasira. Sisanda alimwuliza, "Baba, kuna nini kibaya?"

Babake alieleza, "Leo, kundi la nyuki lilimuuma mama twiga. Kichwa chake kilivimba hadi macho yake ya kupendeza yakazibwa. Tulijaribu kumwokoa, lakini ilikuwa bure. Alikufa. Kinachohuzunisha zaidi ni kwamba alikuwa na ndama mchanga ambaye bado anamhitaji."

5

"Ah, la!" Sisanda alianza kulia. "Heri ningeweza kumsaidia. Labda yule ndama vilevile analia kama mimi."

Sisanda alilia kwa muda mrefu. Mamake alijaribu kumfariji. Alimsomea hadithi moja zaidi wakati wa kulala ili aweze kusahau angalau kidogo uchungu aliokuwa nao kumhusu yule ndama.

Hatimaye, Sisanda alipatwa na usingizi huku akisikiliza sauti ya mamake.

6

Asubuhi iliyofuata Sisanda alikuwa na wazo! Alimwuliza babake, "Ninaweza kwenda kufanya kazi nawe leo? Ningependa kumpelekea mtoto twiga zawadi."

Wazazi wake walitazamana kisha wakatabasamu, "Ndiyo, bila shaka, unaweza kuja nasi."

7

Siku hiyo ilikuwa yenye joto na mawingu. Kila kitu katika hifadhi ya wanyama kilitulia. Sisanda alisema, "Nadhani hakuna jua leo kwa sababu ya huzuni wa mtoto twiga."

Tembo mkubwa aliitazama familia hiyo ikipita. Mamake Sisanda alisema, "Labda anashangaa kwa nini msichana mdogo anaenda kufanya kazi na wazazi wake."

Sisanda aliitkia kwa kichwa. "Atashangaa atakapogundua sababu hasa," Sisanda aliwaza.

8

Walimpata mtoto twiga akiwa peke yake. Alilegeza shingo lake refu na kuinama. Macho yake makubwa yalipumbaa.

Sisanda aliufungua mkoba wake akatoa kitabu. Wazazi wake walishangaa alipoanza kumsomea mtoto twiga. Mtoto twiga aligeuza kichwa chake akatazama kulikotoka sauti ya Sisanda akasikiliza kama aliyelewa kila neno.

Mwanzoni, wazazi walidhani kumsomea twiga ni jambo la ajabu, lakini walibadili mawazo yao walipomwona mtoto twiga akitulia.

9

"Hadithi yangu ilimfariji," Sisanda alimwambia babu yake alipofika nyumbani. Sisanda alienda kumtembelea mtoto twiga kila alasiri na wakati wa wikendi.

Kila alipoenda, alibeba hadithi tofauti kumsomea. Marafiki hao wawili walionekana vizuri pamoja hata watalii waliopita waliwapiga picha.

10

Polepole, mtoto twiga alianza kupata nguvu. Watu waliofanya kazi katika hafidhi hiyo walimlinda vizuri. Upendo kutoka kwa rafiki yake Sisanda, ulifanya miujiza.

Siku moja meneja wa hifadhi alimwuliza Sisanda ampatie rafiki yake mpya jina. "Furaha ni jina nzuri," Sisanda alisema.

11

Siku iliyofuata, meneja wa hifadhi alimpigia simu mwalimu wa Sisanda. Aliwaalika wanafunzi wa darasa la Sisanda kumtembelea Furaha.

Mtoto twiga alikuwa amekua mrefu na mwenye nguvu katika muda wa miezi mitatu tangu Sisanda alipomtembelea mara ya kwanza.

12

Siku ya matembezi, wanafunzi 40 wa darasa la 3 walisubiri kwa hamu kufunguliwa kwa lango la hifadhi.

Sisanda aliwaongoza wote wakaenda kumwona Furaha. Wengine walimtazama yule twiga mrefu kwa mshangao. Wengine walicheka kwa woga.

Bi Keziah, mwalimu wao, alitabasamu tu.

13

"Sisanda, rafiki yako ni mrembo. Umemsaidia sana," mwalimu alisema.

"Anaitwaje?" Mvulana mmoja aliuliza.

"Anaitwa Furaha," Sisanda alimjibu.

Bi Keziah alisema, "Bila shaka anafurahi."

14

Watoto waliketi chini wakamsikiliza Sisanda akisoma hadithi aliyomsomea Furaha siku aliyomtembelea mara ya kwanza.

Meneja wa hifadhi alipiga picha. Baadhi ya watalii waliopita pia walipiga picha.

Mpiga picha kutoka gazeti moja vilevile alipiga picha. Aliwaahidi kuwa picha yao ingechapishwa katika gazeti la mtaa wao hivi karibuni. Kila mmoja alishangilia.

15

Ilikuwa zawadi ya kipekee!

Sisanda kusoma hadithi ili kumponya rafiki.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Zawadi ya Sisanda
Author - Gcina Mhlophe
Translation - Ursula Nafula
Illustration -
Language - Kiswahili
Level - Read aloud