Kwa nini Nzi humsumbua Ng'ombe
Jaco Jacobs
Stephen Wallace

Je, umewahi kuona kundi la ng'ombe malishoni? Kila mara ng'ombe hutikisa kichwa chake. Huonekana akijaribu kuwafukuza nzi wanaomsumbua.

Lakini, kwa nini nzi hupenda kuzunguka kichwa cha Ng'ombe?

1

Inaaminika kuwa tabia hii ilianza zamani katika nchi ya mbali. Malkia wa nchi hiyo alikuwa tajiri na mkarimu.

Siku moja aliamua kuwaandalia wanyama wote karamu. Aliandaa meza kubwa ya nyama, mikate, mboga aina aina na matunda matamu.

2

Wanyama wailfurahia vyakula wakajilamba midomo. Malkia alisema, "Mnyama mkubwa katika kila meza ndiye atakayegawa chakula katika meza hiyo."

Ng'ombe alikuwa ameketi meza moja na Kondoo, Mbuzi, Mbwa, Bata Bukini na Nzi. Ng'ombe akaanza kuwagawia chakula. Alimpa kila mnyama kipande kikubwa cha mkate na jibini.

3

Kwa vile Nzi alikuwa mdogo, Ng'ombe alijifanya
hakumuona.

"Zuum! Zuum! Zii! Na mimi, je? Tafadhali nigawie chakula pia," Nzi alilalamika.

Ng'ombe hakumsikia Nzi. Aliendelea kuula mkate wake. Maskini Nzi aliketi bila chochote huku akiwatazama wanyama wengine wakila.

4

Walipomaliza kula mkate, Ng'ombe aliwagawia nyama na mboga. Kila mnyama alipokea sahani kubwa ya chakula.

Lakini, kwa vile Nzi alikuwa mdogo, Ng'ombe tena hakumuona.

"Zuum! Zuum! Zii! Na mimi, je? Tafadhali nigawie chakula pia," Nzi alilalamika kwa sauti kuliko mara ya kwanza.

Ng'ombe alimkasirikia Nzi.

5

"Eboi! Kumbe huna adabu?" Ng'ombe alimwuliza. "Mdudu mdogo kama wewe hustahili kuwa katika karamu ya malkia. Subiri hadi wanyama wote wakubwa wamalize kula."

Chakula kilikwisha. Maskini Nzi hakupokea hata chembe.

Ng'ombe akaanza kugawa matunda tikiti maji na matofaa.

6

Wanyama wote wakapata chakula isipokuwa Nzi. "Zuum! Zuum! Zii! Na mimi, je? Tafadhali nigawie chakula pia," Nzi alilalamika tena.

Ng'ombe alicheka huku akiuma tofaa. "Ninyi mnasikia chochote?" Aliwauliza wanyama wengine.
"Mimi sijasikia chochote."

Wanyama wote walishiba kupita kiasi isipokuwa Nzi. Tumbo lake lilinguruma kwa njaa.

7

Baada ya chakula, walicheza na kuburudika. Nzi alikuwa amekasirika. Aliamua kurudi nyumbani.

Malkia alimwuliza, "Nzi, mbona unaondoka? Hujafurahia karamu?"

Nzi aliinama kwa heshima, "Samahani, chakula kilikuwa kitamu. Lakini sikugawiwa hata chembe." Nzi alimweleza malkia namna ilivyokuwa.

Malkia alikasirishwa na Ng'ombe.

8

Malkia akasema, "Kutoka leo, wewe na marafiki zako mtakuwa mkiwasumbua Ng'ombe kila siku tangu asubuhi hadi jioni. Utakizunguka kichwa na kupiga kelele karibu na masikio yake.

Hivyo ndivyo atakavyopata funzo. Hatawahi kukudharau tena. Atajua kwamba kwangu mimi, hata mdudu mdogo ni muhimu."

9

Hiyo ndiyo sababu Nzi amekuwa akifanya hadi leo. Yeye na marafiki zake hupiga kelele kwenye masikio ya Ng'ombe tangu asubuhi hadi jioni.

Wanapofanya hivyo, wao huimba "Zuum! Zuum! Zii! Hamtatudharau tena. Semeni ndiyo!"

10
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Kwa nini Nzi humsumbua Ng'ombe
Author - Jaco Jacobs
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Stephen Wallace
Language - Kiswahili
Level - Read aloud