

Mara nyingi, Chui alitaka kumshika Swara.
Swara naye alikuwa akitoroka kila alipomwona Chui.
Siku moja, Chui alimwambia Swara, "Ningependa tuwe marafiki. Unachokula, mimi sili. Hakuna sababu ya kuwa maadui."
Swara alikubali. Chui akasema, "Tule kiapo cha kutufanya marafiki. Atakayeasi, mtoto wake atakufa."
Walikula kiapo cha kuwafanya marafiki.
Usiku, Swara alilala chini ya mti na Chui akalala juu ya mti katikati ya matawi.
Baada ya muda, Swara alinona na Chui alikonda.
Chui alitamani kumla Swara aliyenona. Akasema, "Sina haja na kiapo. Sina hata mtoto!"
Chui alimrukia Swara akajaribu kumshika.
Lakini, hakuweza. Alinaswa kwenye matawi.
Swara alishtuka sana. Aliruka juu akaanza kulia, "Bee! Bee!"
Chui akamsihi, "Rafiki yangu, nisaidie. Tulikubaliana kuwa atakayevunja kiapo chetu, atampoteza mtoto wake."
Swara alimjibu, "Inaonekana kuwa wazazi wako ndio waliokula kiapo. Sasa wewe ndiwe utakayekufa."

