

Miaka mingi iliyopita, Jua na Maji walikuwa marafiki.
Wote waliishi duniani.
Jua alipenda kumtembelea Maji mara kwa mara.
Lakini, Maji hakuwahi kwenda kumtembelea Jua.
Mwishowe, Jua alimwuliza Maji kwa nini hakuenda kumtembelea.
Maji alijibu kwamba Jua ana nyumba ndogo sana. Alisema, "Nikija na familia yangu, tutakutupa nje."
Maji alisema, "Ukitaka nikutembelee, jenga uwanja mkubwa. Watu wangu ni wengi mno. Wao huchukuwa nafasi kubwa."
Jua alirudi nyumbani kwa mkewe, Mwezi. Mwezi alimsalimu kwa tabasamu kubwa.
Kisha Jua akamwambia Mwezi kuhusu ahadi aliyompa Maji.
Siku iliyofuata, Jua alianza kuandaa uwanja mkubwa ambamo angemtumbuiza rafiki yake, Maji.
Uwanja ulipokuwa tayari, alimwalika Maji awatembelee.
Maji alipofika, alimwuliza Jua iwapo ingekuwa salama yeye kuingia ndani.
Jua alijibu, "Ndiyo, ingia rafiki yangu."
Maji akaanza kutiririka ndani ya nyumba!
Aliambatana na mamba, samaki, vyura, nyoka, konokono, na wanyama wote wa majini.
Muda mfupi baadaye, Maji alifika magotini. Alimwuliza Jua iwapo bado ilikuwa salama.
"Ndiyo," Jua alijibu tena.
Jamaa wengine wengi wa Maji wakaendelea kuingia.
Maji alifika kiwango cha upeo wa kichwa cha mtu. Alimwambia Jua, "Je, watu wangu zaidi wanaweza kuja?" Jua na Mwezi walijibu, "Ndiyo."
Maji alitiririka ndani zaidi hadi Jua na Mwezi wakalazimika kuning'inia kwenye paa.
Watu wa Maji waliendelea kuingia hadi wakafika juu ya paa la nyumba. Jua na Mwezi walilazimika kwenda juu angani.
Tangu wakati huo, Jua na Mwezi huishi angani.

