

Hapo zamani, katika kijiji kimoja, kulikuwa na mvulana aliyeitwa Roba.
Roba alikuwa rafiki ya Leah. Walikuwa majirani.
Siku moja, walienda kuchota maji.
Walipokaribia kisima, walimwona ng'ombe akiwa amelala hapo.
Waliketi chini kujadiliana vile wangecheza naye.
Roba alianza kumuiga ng'ombe. Alisema kwa sauti ya juu, "Mooo, mooo, moooooo!"
Aliendelea hadi ng'ombe akawatazama. Leah alishtuka.
Roba aligundua kwamba Leah alikuwa ameogopa.
Roba alisema, "Twende tumpige atoroke ili tuchote maji."
Leah alimjibu huku akitetemeka, "Roba, ninaogopa!"
Roba alikuwa wa kwanza kuenda. Leah alimfuata
polepole.
Walijaribu kumgonga ng'ombe, lakini ng'ombe yule hakusonga.
Roba alisema, "Leah, unaweza kuketi hapa. Mimi nitachota maji."
Leah alikubali.
Roba alijaza ndoo ya kwanza maji.
Alipokuwa akijaza ndoo ya pili, ng'ombe alisimama.
Alimuenua Roba juu kwa pembe moja kisha akamtupa mgongoni.
Roba alipiga kelele, "Joo, jooo, jooooo!"
Leah aliangua kicheko na hakuweza kuacha kucheka.
Ng'ombe alisema, "Mooo, mooo, moooooo!"
Leah alipoacha kucheka, alikimbia haraka alivyoweza.
Alimpata mamake Roba akifagia.
Alisema huku akihema, "Ma-ma! Ma-ma! Ng'o-mbe amemchukua Roba!"
Mamake Roba aliangusha ufagio akakimbia.
Unadhani ni nini kilichotendeka baadaye?

