

Hapo kale, kulikuwa na mtu aliyeitwa Pepe. Aliishi katika mtaa wa Umoja.
Pepe aliishi na mbwa wake katika chumba chake kidogo.
Siku moja Pepe alikuwa mgonjwa. Hakuwa na yeyote wa kumsaidia.
Alipopata nafuu, aliamua kumwoa mwanamke aliyeishi hapo karibu.
Pepe aliwaalika marafiki na jamaa zake kuhudhuria harusi.
Alichangamka sana akidhani kuwa amempata msaidizi.
Bi harusi alipatiwa vikapu vya wimbi, mikeka, ndizi, njugu, na zawadi nyingine.
Baada ya sherehe ya harusi, wageni waliondoka kurudi makwao.
Pepe alikuwa tayari kuanza maisha mapya pamoja na mkewe na mbwa wake.
Siku iliyofuata, Pepe alimwandalia mkewe ndizi tamu, lakini alikataa kuzila.
Lakini Pepe alipokwenda kuwinda, mwanamke huyo alizila ndizi zote.
Baadaye Pepe aliporudi kutoka mawindoni alihisi njaa. Alitaka kuzila zile ndizi tamu.
Mkewe alimwambia kuwa mbwa alizila zote!
Siku iliyofuata, Pepe alikwenda shambani.
Aliporudi, alipata kuwa mkewe alikuwa ameila nyama yote. Hakumgawia hata mbwa.
Siku nyingine, Pepe alikwenda kumtembelea rafikiye.
Aliporudi, mkewe alikuwa amezila njugu zote. Kikapu kilikuwa kitupu. Pepe alimkasirikia sana mkewe.
Pepe aligundua kuwa mwanamke huyo alikuwa na shida. Aliamua kumnasa.
Aliweka maziwa katika chungu cha ajabu kisha akakiweka mvunguni. Akaondoka kwenda kuwinda.
Mwanamke alikiona chungu kilichokuwa kimejaa maziwa. Alikichukua akakiweka mdomoni. Aliyanywa maziwa yote huku mbwa akimtazama.
Kwa bahati mbaya, chungu kilikwama mdomoni. Alijaribu kukiondoa, lakini ilikuwa bure. Alipiga kelele na kuruka juu na chini.
Chungu kilikwama pale pale. Mbwa alitazama haya yote.
Mbwa alikimbia kumtafuta Pepe. Alibweka, akabweka, akaruka juu na chini.
Pepe alifahamu kuwa kulikuwa na jambo mbaya nyumbani.
Walikimbia pamoja kwenda nyumbani. Pepe alistaajabu kumpata mkewe na chungu mdomoni.
Akamtazama kwa mshangao.
Pepe alimgusa mkewe kwenye shavu na chungu
kikaanguka mara moja.
Mwanamke huyo aliaibika sana akaamua kurudi kwa wazazi wake.

