Mbuzi, mfalme bandia
Alice Nakasango
Marleen Visser

Hapo zamani, kulikuwa na mbuzi aliyeitwa Ibego.
Ibego alikuwa mfalme wa mifugo na ndege. Aliishi maisha mazuri.

Siku moja, Ibego aliwaita mifugo wote na ndege mkutanoni.

1

"Rafiki zangu, nimewaita kwa sababu niliota ndoto," Ibego alisema.

Mifugo wote na ndege walimsikiliza mfalme wao kwa makini.

2

"Niliota kuwa kulikuwa na njaa na ukosefu wa maji katika nchi yetu. Wengi wa jamaa zetu walifariki!" Mfalme alisema.

Mifugo na ndege waliposikia ndoto ile, walijawa na hofu. "Tutafanyaje?" Paka aliuliza.

3

Kuku na Bata walikuwa na wazo. Walisema, "Kila mmoja wetu alete chakula kiwekwe katika hifadhi ya mfalme."

Mifugo wote na ndege walikubaliana na wazo hilo.

4

Mfalme alitoa sharti moja. Alisema, "Yeyote atakayekosa kuleta chakula, mtamfunga mumlete kwangu."

5

Wakati wa mfalme Mbuzi kustaafu ulifika. Mifugo wote na ndege walikutana kumchagua mfalme mpya.

Paka alichaguliwa kuwa mfalme wao mpya.

6

Mbuzi hakumtambua Paka kama mfalme.

Alisema, "Mimi ndiye mfalme na hakuna mwingine. Siwezi kumtii mwingine yeyote."

7

Mifugo walipeleka chakula katika hifadhi ya mfalme wao mpya. Mbuzi hakupeleka chochote.

Ng'ombe alisema, "Mbuzi alipokuwa mfalme, tulimtii. Hataki sasa kumtii mfalme wetu mpya. Tufanyeje?"

8

Mifugo wote na ndege walikasirika. "Kwani anadhani yeye ni tofauti nasi?"

Walinung'unika.

9

Mbwa alisema, "Nilimsaidia alipokuwa mfalme. Sikuwa nikilala usiku. Kila wakati nilikuwa naye, tayari kumsaidia."

10

Kondoo alisema, "Nilimpatia sufu yangu ili awafunike wanawe."

11

Nguruwe naye alisema, "Alipokuwa mfalme, aliwaambia marafiki zake kuwa mimi ni mlafi. Lakini nilitumia muda mwingi kuitunza bustani yake na kupalilia mawele na mahindi."

12

Kondoo aliuliza, "Eti alisema nini? Kwamba wewe ni mlafi? Alifikiri kuwa atakuwa mfalme milele?

Lazima afahamu kuwa yeye si mfalme tena. Hata sijui kwa nini anafikiri kuwa yeye ni muhimu sana."

13

Mifugo wote walicheka na kukubaliana kwamba lazima Mbuzi apeleke chakula kwa mfalme mpya.

Mfalme Paka alimwamuru Mbuzi aende kwake.

14

Mifugo walipoenda, walimkuta Mbuzi akistarehe.

"Siendi kwa Paka. Hakuna mfalme mwingine ila mimi. Ukiwa mfalme, unasalia mflame," Mbuzi alisema kwa kiburi.

15

"Basi tutakufunga kwa kamba tukupeleke kwa mfalme mpya," Kondoo alisema.

16

Ng'ombe alimfunga Mbuzi akamvuta na kumpeleka kwa mfalme.

Kondoo, Bata, Mbwa, Nguruwe na Jogoo walimshangilia Ng'ombe wakisema, "Mpeleke huyu mbuzi kaidi kwa mfalme mpya!"

17

Tangu wakati huo, kila mbuzi hukataa kusonga anapovutwa.

Hufikiri kuwa anapelekwa kwenye mahakama ya mfalme.

18
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mbuzi, mfalme bandia
Author - Alice Nakasango
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Marleen Visser
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs